LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jun 4, 2020

KINANA AONYESHA UKOMAVU KATIKA SIASA, AMUOMBA RADHI MWENYEKITI WA CCM RAIS DK. MAGUFULI

CCM Blog, Arusha
Katibu Mkuu Mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Abdulrahaman Kinana (pichani) amemuomba radhi Mwenyekiti wa CCM Rais Dk. John Magufuli kwa kauli mbalimbali alizotoa hadi Chama kulazimika kumpa adhabu hivi karibuni.

Kinana alitoa tamko la kumuomba radhi Mwenyekiti wa CCM, Rais Dk. Magufuli, alipozungumza na Waandishi wa habari baada ya kukutana na Mwenyekiti wa CCM wa mkoa wa mkoa huo Zelothe Stephen na kufanya mazungumzo naye katika ofisi za CCM mkoa wa Arusha leo.

Katika tamko lake la kuomba radhi Kinana alisema yafuatayo;-

"Najua nilikereka wakati fulani na nilihuzunika na nilikasirika katika kushughulikiwa lile swala nadhani nilienda mbali kidogo nikasema maneno ambayo hayakuwa mazuri kwa viongozi wangu na Mwenyekiti wa Chama na Rais, baada ya kutafakari nadhani naweza kusema ni wakati mwafaka ni wakati mzuri nami kuungana nao na kumtaka radhi na kumuomba msamaha, nikasema Mwenyekiti nimekukwaza na nimekukera na nimekuudhi.

Wala si Mwenyekiti peke yake kuna na wanachma na Watanzania ambao labda walisema ahh, mbona Ndugu Kinana amekwenda mbali kiasi hicho?, labda kwa kupitia kwake vilevile na wale waliohuzunishwa na kusikitishwa niwaombe radhi. Lakini hasahasa nadhani  nimuombe radhi  Mwenyekiti na Rais kwa yale ambayo niliyasema.

Na unajua misahafu yetu lakini vilevile katika maisha ni uungwana wakati mwingine kukaa na kutafakari na kuomba radhi na sina shaka hata kidogo leo akinisikia nikisema hayo bila shaka ataniwia radhi.

Unajua kwenye Chama utaratibu wa hukumu na kupeana adhabu ni utaratibu wa kawaida na mimi sikuwa wa kwanza kuna viongozi wengi na bahati nzuri au mbaya wengi wanaoadhibiwa ni viongozi wa Chama si wanachama wa kawaida ni watu wazitowazito hivi kwa hiyo na mimi nimepata adhabu kama walivyopata wengine.

Hata mimi huko nyuma niliwahi kushiriki katika kutoa adhabu kwa wengine kwa hiyo you know,... nina hakika mimi sitakuwa wa mwisho kupewa adhabu kwa sababu chama kinaendelea, chama kipo na viongozi wapo na watajikwaa na wakijikwaa nao watapata adhabu, nakadhalika", amsema Kinana.

Kinana akiwa na baadhi ya viongozi wa chama walipewa adhabu  baada ya mazungumzo yao ya simu yaliyonaswa na kuwekwa katika mitandao ya simu wakimteta Mwenyekiti wa Chama Rais Dk. Magufuli na kusababisha uongozi wa CCM kuwaita na kuwahoji viongozi hao mbali na Kinana akiwemo Katibu Mkuu mstaafu wa CCM Yussuf Makamba na Benard Membe.

Wengine waliokuwemo katika sakata hilo ni Januari Makamba, Katibu Mwenezi mstaafu wa CCM Nape Nnyauye na William Ngeleja ambao wao walimuomba radhi mapema Rais Dk. Magufuli kabla ya kuitwa ili kuhojiwa na Chama.

Hatua ya Kinana kumuomba Rais imeelezewa na wana CCM na Watanzania mbalimbali kwamba ni ishara ya ukomavu wa kisiasa na fundisho kubwa kwa wana CCM wenyewe hasa wanaochipukia .

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages