LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Mar 23, 2020

MBARONI KWA TUHUMA ZA KUMUUA MPENZI WAKE NA KUJARIBU KUJIUA

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia mbebamizigo mmoja Festo Maduhu mwenye umri kati ya miaka 28 na 30 Mkazi wa Mtaa wa Benki Kabwe Jijini Mbeya kwa tuhuma za kumuua mpenzi wake kisha na yeye kujaribu kujiua kwa kisu.

Ni kwamba mnamo tarehe 22/03/2020 majira ya saa 09:00 Asubuhi huko katika nyumba ya kulala wageni iitwayo “NEGERO” iliyopo Mtaa wa Ilolo, Kata ya Ruanda, Tarafa ya Iyunga, Jijini Mbeya katika chumba namba 111 @ Victoria, Mwanamke mmoja aitwaye JESCA MICHAEL @ KUNGULU [28] Mhudumu wa Nyumba ya Kulala Wageni na Baa na Mkazi wa Ilolo Jijini Mbeya aligundulika kuuawa kwa kukabwa shingo na kupigwa sehemu za usoni na mtuhumiwa FESTO MADUHU ambaye ni mpenzi wake.

Kiini cha tukio hili ni wivu wa kimapenzi kwani mtuhumiwa alikuwa anamtuhumu marehemu kuwa alikuwa na mahusiano na mwanaume mwingine ambaye jina linahifadhiwa kwa sababu za kiupelelezi na ufuatiliaji.

Katika ufuatiliaji wa kumkamata mtuhumiwa mara baada ya tukio hilo, mtuhumiwa alikutwa akiwa amejifungia nyumbani kwake na baada ya askari kuvunja mlango wa nyumba hiyo alikutwa akiwa anaendelea kujichinja koromeo lake kwa kutumia kisu ambapo askari Polisi walimuokoa na kumpeleka Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya kwa matibabu.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya kwa uchunguzi zaidi wa kitabibu. Aidha mtuhumiwa anaendelea kupatiwa matibabu kitengo cha dharura Hospitalini hapo akiwa chini ya ulinzi na mara apatapo nafuu atahojiwa na kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma za Mauaji na kujaribu kujiua.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi ULRICH MATEI anatoa wito kwa jamii kuacha kujichukulia sheria mkononi. Aidha anatoa wito kwa jamii kuacha tabia ya kupuuzia migogoro ya aina yoyote baina ya mtu na mtu au kikundi cha watu na badala yake watoe taarifa mapema sehemu husika likiwemo Jeshi la Polisi kwa hatua zaidi za kisheria.

Imetolewa na:
(ULRICH O. MATEI -SACP)
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages