LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 12, 2020

MWANAFUNZI AFARIKI KATIKA JARIBIO LA KUTOLEWA MIMBA

Na Lydia Lugakila Kagera:-

Kufuatia mwanafunzi wa miaka 14 wa darasa la sita manispaa ya Bukoba mkoani kagera kufariki dunia baada ya jaribio la kutoa mimba  kamanda wa polisi mkoani Kagera Revocatus Malimi amewataka wananchi mkoani humo  kuachana na kupata huduma za afya mtaani badala yake waende sehemu ambazo zimeruhusiwa kisheria ambako kuna watalamu wazoefu.

Kauli hiyo imetolewa na kamanda Wa polisi mkoani Kagera Revocatus Malimi wakati akiongea na waandishi wa habari juu ya matukio mbali mbali yakiwemo ya kujinyonga.

Kamanda Malimi amesema kuwa jamii inapaswa kuondokana na dhana ambazo zinaleta madhara ikiwa ni pamoja na kupata huduma za afya mtaani jambo ambalo ni hatari kwa maisha ya watu kutokana na baadhi ya watoa huduma kutokuwa wazoefu sambamba na elimu juu ya tiba wazitoazo.

Akieleza tukio la mwanafunzi aliyefariki dunia baada ya jaribio la kutolewa mimba kamanda Malimi amesema mnamo Februari 8 mwaka huu majira ya saa sita katika mtaa wa kilima hewa katika Kata ya Nyakato nyumbani kwa Vedastina Cleophace manispaa ya Bukoba mkoani humo imedaiwa kuwa mwanafunzi Alinda Revelian darasa la sita katika shule ya msingi kilima amefariki dunia baada ya kufanyiwa jaribio la kutolewa mimba.

Kamanda huyo wa polisi amesema siku ya tukio maehemu alikwenda nyumbani kwa Dezdery Solomon Kahwa(49) mkazi Wa mtaa wa Kibengwe manispaa ya Bukoba ambaye amewahi kuajiriwa na kufanya kazi ya Muuguzi katika Zahanati ya Buzi na baadae kufukuzwa kazi serikali katika zoezi la kuondoa watumishi hewa waliojipatia kazi kwa kutumia vyeti vya kugushi na baadae akaendelea kuhudumia wagonjwa mtaani bila kibali na kwa kificho.

Ameongeza kuwa marehemu alikwenda nyumbani kwa mtuhumiwa ambako inadaiwa alipatiwa matibabu ya maumivu ya tumbo kitendo kilichowafanya ndugu na jamaa kubaini hali ya kifo hicho.

Aidha mtuhumiwa amekamatwa na kuhojiwa na jeshi hilo na mwili Wa marehemu umefanyiwa uchunguzi na Daktari Wa binadamu katika hospitali ya Rufaa Bukoba ambaye amebaini chanzo cha kifo hicho kuwa ni kutobolewa kwa mfuko wa uzazi na kuingiziwa madawa sumu katika jaribio la kutoa mimba.

Kutokana na hali hiyo jamii imehaswa kuacha Mara moja kuamini tiba za mitaani ambazo husababisha vifo kwa watoto.

Katika hatua nyingine kamanda huyo amemtaja mwanafunzi Buberwa Mberwa (14) mwanafunzi Wa darasa la tano shule ya msingi Kahororo mkazi Wa mtaa wa Rwazi kukutwa amejinyonga kwa kujitundika kwenye nondo za dirisha kwa kutimia mkanda Wa begi ambao alikuwa akitumia kama mkanda Wa suriali lake.

Hata hivyo amehasa jamii kutumia njia sahihi kutatua changamoto za maisha badala ya uamuzi wa kujiua ambazo siyo tu husababisha matatizo katika familia wanayoacha kutokana na kukatiza ndoto zao na za wazazi lakini pia makosa katika dini zote duniani na ni uhalifu pia.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages