LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Oct 31, 2019

MKUTANO WA MAWAZIRI WA AFYA NA UKIMWI, SADC KUJADILI NAMNA YA KUIMARISHA SEKTA YA AFYA


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu, kwa Waandisahi wa Habari na Wataalmu wa Afya Kutoka Wizara ya Afya (Hawapo pichani) kuhusu Mkutano wa Mawaziri wa Afya na Ukimwi kwa nchi za SADC, utakaofanyika kuanzia Novemba 04 hadi 08, 2019 katika ukumbi wa Banki Kuu ya Tanzania Jijini Dar es Salaam, kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari-MAELEZO(Uratibu-Mawasiliano Serikalini) Bi. Zamaradi Kawawa wa (kwanza) na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Zainabu Chaula.

  NA PASCHAL DOTTO-MAELEZO.

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Mawaziri wa Sekta ya Afya na UKIMWI kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) unaotarajiwa kufanyika nchini kuanzia Novemba  04 hadi 08, 2019, katika  Ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika Mkutano na Waandishi wa Habari, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe.Ummy Mwalimu amesema kuwa Mkutano huo utafunguliwa rasmi na  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, huku kauli mbiu yake ikiwa ni “Ushirikiano wa nchi za SADC ni nguzo kuu kufikia Maendeleo Endelevu ya Sekta ya Afya na Mapambano dhidi ya UKIMWI.

Mhe. Ummy amesema kuwa katika Mkutano huo ambao kwa kiasi kikukubwa utawakutanisha Mawaziri wa Afya na Watendaji Wakuu wa Idara za Afya kutoka Nchi Wanachama wa SADC takribani 200 utakuwa na lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayoikumba sekta ya Afya Ukanda huo wa Afrika.

“Mkutano wa Mawaziri wa Sekta ya Afya na UKIMWI unalenga kuangalia hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Itifaki ya Afya ya SADC ya mwaka 1999 na Mpango Mkakati wa Kanda kuhusu masuala ya Afya, na pia kutakuwepo na ajenda za kuwezesha ujenzi mpya wa Sekta ya Afya kwa Nchi Wanachama”, Alisema Waziri Ummy.

Alizitaja ajenda hizo kuwa ni  pamoja na Magonjwa ya kuambukiza yanayoziathiri nchi za SADC kama vile Kifua Kikuu, Malaria na UKIMWI; Masuala ya lishe hususani uongezaji virutibisho na lishe ya makuzi kwa watoto, uzito uliopitiliza na viribatumbo na huduma ya Lishe wakati wa majanga

Ajenda nyingine ni uimarishwaji wa Mifumo ya Afya ikiwemo uimarishaji wa upatikanaji wa dawa, na upatikanaji wa takwimu za afya, rasilimali watu, rasilimali fedha na Masuala ya ununuzi wa pamoja wa dawa na vitendanishi ili kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za manunuzi kwa nchi wanachama, na hiyo itasaidia kuimarishwa kwa Sekta ya Afya huku Tanzania ikiwa mbele kwenye masuala ya ununuzi wa dawa baada ya Bohari Kuu ya Dawa(MSD) kuchaguliwa kuwa mzabuni katika  ununuzi wa dawa kwa nchi za SADC.

Aidha Waziri Ummy alisema kuwa katika kuimarisha afya ya Mama na Mtoto suala la kuimarisha huduma za Afya kwa uzazi salama pamoja na chanjo ya mtoto ni suala lingine ambalo linazikumba nchi hizo, kwa hiyo mjadala utajikita katika  suala hilo ili kulinda Afya ya Mama na Mtoto hilo.

Kwa upande wa magonjwa ya mlipuko, majanga ya dharura ikiwemo  magonjwa ya milipuko kama vile Ebola ambayo tayari yanazikumba nchi wanachama kama vile Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Uganda masuala haya yatajadiliwa kwenye mkutano ili kupata ufumbuzi zaidi.

“Wizara yangu ikiwa ni Mwenyekiti wa Mkutano huu itasimamia hoja zake katika masuala mbalimbali ya afya ikiwa ni pamoja na kuzishauri nchi wanachama kuwekeza katika afya bora ambayo ndiyo msingi wa maendeleo na ukuaji wa uchumi; nchi wanachama kuendelea kukabiliana na magonjwa yanayozuilika na nchi wanachama kuwa na huduma za afya zenye usawa kwa watu wote”, Alisema Waziri Ummy.

Mbali na kushiriki Mkutano huo, Mawaziri watapata fursa ya kufanya ziara katika maeneo ya kimkakati ikiwemo; Kiwannda cha Viuadudu vya Malaria cha Labiofam kilichopo Wilayani Kibaha, Mkoani Pwani tarehe 8 Novemba 2019,  lengo la ziara hiyo ikiwa ni kuzindua rasmi siku ya Malaria ya SADC na Kampeni ya Kitaifa ya Kupambana na Malaria inayojulikana kama “Zero Malaria Starts with me” pamoja na kukitangaza kiwanda hicho kwenye nchi wanachama wa SADC ili kupata soko la dawa zinazozalishwa kiwandani hapo, pia watatembelea Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kufuatia ushindi wake wa zabuni ya ununuzi, utunzaji,na Usambazaji dawa na vifaa Tiba wa Nchi wanachama wa SADC.

Mtaalamu wa Chakula na Lishe kutoka Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Bi. Grace Moshi akieleza jinsi hali ya lishe duni inavyosababisha viribatumbo na utapiamulo kwa watoto na watu wazima, moja ya Ajenda itakayojadiliwa kwenye Mkutano wa Mawaziri wa Afya na Ukimwi kwa nchi za SADC, utakaofanyika kuanzia Novemba 04 hadi 08, 2019 katika ukumbi wa Banki Kuu ya Tanzania Jijini Dar es Salaam.


Mtaalamu wa Mpango wa Kudhibiti UKIMWI kutoka Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Zeye Masunga, moja ya Ajenda itakayojadiliwa kwenye Mkutano wa Mawaziri wa Afya na Ukimwi kwa nchi za SADC, utakaofanyika kuanzia Novemba 04 hadi 08, 2019 katika ukumbi wa Banki Kuu ya Tanzania Jijini Dar es Salaam.

1 comment:

  1. Wakubwa wanasema dunia imepunguza kasi ya mapambano dhidi ya malaria katika kipindi cha miaka mitano ya sasa (2015 - 2019) ikilinganishwa na miaka kumi kabla (2005 -2015) na hii inadhihirishwa na idadi ya watu wanaoshambuliwa na kupoteza maisha kwa ugonjwa wa malaria. Hata hivyo upo ukinzani wa kitakwimu unaoonyeshwa na viongozi wetu kuhusu kupungua kwa maambukizi na vifo kutokana na Malaria. Wachambuzi wa takwimu wako wapi watuambie ukweli? Takwimu za Ukimwi zilikuja kwa kutisha na kuleta taswira ya uoga. Kama hizo hazitoshi, tuliona mgogoro mkubwa wa kitakwimu kati ya mwaka 1990 hadi 2010 tulipoambiwa wanawake 572 wanapoteza maisha kutokana na matatizo ya kuzaa licha ya kuwa jitihada kubwa zilionekana wazi zikifanywa na Serikali na wadau wake. Tumeona takwimu za uharibifu wa mazingira eti miti inakatwa na kufyekwa na kusababisha hekta 400,000 kupotea kila mwaka takwimu hizi tuliziona tangu mwaka 1996 lakini zimebaki hizohizo hadi mwaka huu tunaposikia hekta 800,000 kuteketezwa kila mwaka...Kwanini takwimu? Takwimu mbovu zinapotosha jamii, watengeneza mipango, viongozi na zaidi wanasiasa kwani inakuwa kazi kuendesha mapambano ukiwa na data zenye udhaifu. Kwa maoni yangu natamani kuona Serikali inawekeza katika utafiti, inatenga fedha za utafiti, inatayarisha watafiti mahiri na inatumia tafiti za wanafunzi na wakufunzi wa taasisi za elimu ya juu na asazi zisizo za kiserikali na kisha kufanya uchambuzi na kufikia muafaka. Maeneo ya kipaumbele kwa nchi za SADC iwe takwimu za kiafya hasa utapiamlo, Ukimwi, Malaria, Ebola, TB na pia mazingira kwa kuangalia vyoo, upatikanaji wa maji safi na salama, hali na tabia nchi ya mabadiliko, mazalia ya mbu na wadudu wanaosababisha magonjwa ya mlipuko kama dengue na jamii yake hasa yanayotokea India kuja Tanzania. Vinginevyo, tuanzishe mijadala ya muda mrefu kuhusu magonjwa yanayozuilika, yanayotibika na yanayosababisha madhara makubwa kwa binadamu. Isije kuonekana hakuna kazi inayofanyika, ikibidi tufunge kwa maombi na sala, tufanye kazi usiku na mchana tupambane na Malaria na nguvu zetu tuelekeze huko kuondokana na mifumo ya "mazoea as usual syndrome". Hongera Waziri na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, kazi yenu inatia matumaini kwamba hapa hakuna kulala mpaka kieleweke. Au mwenzangu unasemaje?
    Daniel Benno Msangya, Ni Balozi wa Mapambano kwa njia ya Habari wa Nchi 11 Duniani zinazoathirika kwa malaria ikiwemo India na nchi 10 za Afrika na Tanzania ikiwemo.Hupatikana kwa 0755893303 benno.apondo@gmail.com

    ReplyDelete

Tupia Comments👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages