Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, katika kipindi cha miezi 14 iliyopita, Marekani imetekeleza vikwazo vikali kabisa dhidi ya taifa la Iran, hata hivyo imeshindwa katika nyanja zote iwe ni katika uga wa kijamii, kisiasa na kadhalika.
Rais Rouhani alisema hayo jana katika hadhara kubwa ya wananchi wa Shirvan, mkoani Khorasan Kaskazini huko kaskazini mashariki mwa Iran na kuongeza kuwa, licha ya Marekani kulitwisha taifa hili vikazo vikali kabisa katika kipindi cha miezi 14 iliyopita, lakini taifa shujaa la Iran, lenye umakini na kusimama kidete mfumo wa Kiislamu katika kipindi chote hiki kumeifanya Washington ishindwe katika njama zake hizo.
Rais wa Iran ameeleza kwamba, Wamarekani wameshindwa kufikia malengo yao katika nchi za eneo kama Afghanistan, Iraq, Syria na Yemen na kama atatokea mtu na kudai kwamba, Iran imetetereka kupitia mashinikizo iliyoandamwa nayo, basi atakuwa amesema urongo na kutamka maneno yasiyo sahihi.
Kadhalika Rais Rouhani amesema kuwa, licha ya mashinikizo ya Marekani, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katu haijanyoosha mkono wa msaada kwa madola ajinabi na mifuko ya kimataifa bali kwa kujitegemea yenyewe, imeweza kulipa hata sehemu ya madeni yake ya mwaka jana.
Rais Rouhani ameashiria pia hatua ya kuendelea kutengwa Marekani katika uga wa kimataifa na kusema kuwa, ukiachilia mbali taifa moja au mawili, nchi zote wanachama wa Bodi ya Magavana ya Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Nyuklia (IAEA) katika kikao chao cha hivi karibuni zilipuuza njama za Washington dhidi ya Iran.
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇