Msemaji wa Ikulu ya Marekani (White House) amesema kuwa, rais wa nchi hiyo hana nia mbaya katika maandishi yake aliyoandika kwenye mtandao wa Twitter kuhusu mbunge Muislamu wa Congress.
Sarah Sanders alisema hayo jana katika mahojiano aliyofanyiwa na televisheni ya ABC News na kudai kuwa, Donald Trump hana nia mbaya na Ilham Omar na wala mtu mwingine yeyote.
Hata hivyo, vitendo na matamshi ya chuki ya Trump dhidi ya watu mbalimbali hasa wageni na hasa hasa Waislamu yanamsuta msemaji huyo wa Ikulu ya Marekani.
Katika ujumbe wake kwa njia ya Twitter, Trump amedai kuwa Ilham Omar, mbunge Muislamu wa Baraza la Congress eti anayadharau mashambulizi ya Septemba 11 huko Marekani.
Wapinzani wa Trump wanaamini kuwa, rais huyo wa Marekani amepotosha na kuyafasiri vibaya kwa makusudi matamshi ya Ilham Omar kwa lengo la kuchochea hisia za chuki dhidi ya Waislamu.
Msemaji wa Ikulu ya Marekani pia amesema kuwa, hatua ya Trump ya kusifu na kuunga mkono mambo yaliyofichuliwa na mtandao wa WikiLeaks wakati wa kampeni za uchaguzi wa mwaka 2016 huko Marekani ilikuwa ni matani na masikhara tu.
Wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais wa Marekani, mwaka 2016, Trump alitegemea sana mambo yaliyofichuliwa na mtandao wa WikiLeaks kuwabomoa wapinzani wake. Hata hivyo hivi karibuni Trump alitia ulimi puani na kudai mbele ya waandishi wa habari kwamba hajui chochote kuhusu mtandao wa WikiLeaks
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇