LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 17, 2019

CCM YAUMWAGIA SIFA MSWADA MPYA WA VYAMA VYA SIASA

Chama cha Mapinduzi (CCM) kimesema wanaodhani kuwa chama hicho kinataka mabadiliko ya sheria ya vyama vya siasa ili nchi irudi kwenye mfumo wa chama kimoja wanakosea.


Akizungumza na wanachama wa CCM mkoani Dodoma leo katika mkutano wa kukusanya maoni kuhusu Muswada wa sheria ya Vyama vya siasa, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dkt.Bashiru Ali amesema mfumo wa vyama vingi umeiimarisha CCM.

"Sheria hii si ya kwanza kutungwa na haitakuwa sheria ya mwisho...Ukiendesha siasa kwa urasimu hutatenda haki", amesema.

Amebainisha kuwa wanatetea muswada huo kwasababu umeongeza uhakika wa utawala na kulinda misingi ya utaifa.

"Mimi natamani sana kwenye sheria hii hata koma(alama ya nukta) isiondolewe lakini mnaweza kutoa maoni yenu ya kuboresha ambayo hayaondoi maudhui", amesema Dkt. Bashiru na kuongeza;

"Kuna mbabaishaji mmoja sitaki kumtaja jina alikimbia chama fulani akisema wanatumia vibaya ruzuku lakini leo tunaleta muswada wa kudhibiti ruzuku kwa vyama anapinga tena, huyu ni mtayarishaji.

Dk Bashiru amewataka wana CCM kuujadili muswada kwa nia njema kwani unakwenda kuimarisha siasa za Tanzania na kuweka imara vyama vya siasa na vinavyotaka kuanzishwa.

"Lakini msiwe na wasiwasi, mashine zimetegwa tayari kinachosubiriwa ni kuanza kazi tu wala si kusubiri, tuko imara kisiasa na chama chenu kiko imara kuliko wakati mwingine," amesema.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages