LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 16, 2018

WAZIRI JAFO ATOA MAAGIZO KWA WAKURUGENZI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo amewataka  wakurugenzi watendaji wa halmashauri kuepuka kujiingiza katika ugomvi wa kisiasa utakaokuwa chanzo cha kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kazi.

Jafo akizungumza na wakurugenzi watendaji wapya wa halmashauri jijini Dodoma jana, aliwataka kuepuka kujiingiza katika makundi ya kisiasa na ugomvi usioeleweka ambao utawafanya kushindwa kutekeleza majukumu yao.

Wakurugenzi hao jana walikula kiapo cha ahadi ya uadilifu kwa watumishi wa umma.

“Simamieni mipaka yenu ya kazi, kila mtu akisimamia mipaka yake kutakuwa hakuna migongano. Ninyi mnaenda huko kwa ajili ya utekelezaji wa ilani ya CCM na hakuna mjadala mwingine,” alisema.

Waziri Jafo alisema, “Msiende kujiingiza katika makundi ya kisiasa na magomvi yasiyoeleweka inawezekana huko mnakokwenda kuna makundi ya kisiasa yanayogombana. Inawezekana huko mnakoenda kuna watu wanagombana simamieni ilani.

“Leo hii unaenda katika halmashauri unamkuta mkurugenzi kivyake, mwenyekiti wa halmashauri kivyake, mbunge kivyake, wakuu wa wilaya kivyao.”

Alisema jambo hilo linafanya halmashauri nayo kwenda kivyake, hivyo utekelezaji wa ilani kuwa mgumu. Alisisitiza uhusiano mwema kazini na ushirikiano akisema, “Kuna baadhi ya watumishi wewe umefika pale ni mgeni, mtu mwingine anakupiga dozi ya sumu iliyokolea hata wengine huwajui kwa sura unaanza kuwachukia.”

Aliwaagiza kutenda haki kwa watu wote na kusimamia miradi ya maendeleo, ukusanyaji wa mapato na kuhakikisha hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zinajibiwa kwa wakati.

Juzi, Jafo alikemea tabia ya baadhi ya wakuu wa wilaya kutumia vibaya mamlaka waliyonayo na kuwaweka watu ndani, akisema inasababisha wananchi kuichukia Serikali.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages