LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jun 19, 2018

WABUNGE WAIKUBALI BAJETI YA SERIKALI

Na Jonas Kamaleki-MAELEZO, Dodoma
Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamezidi kuiunga mkono bajeti ya serikali iliyowasilishwa bungeni mapema wiki liyopita.

Akitoa maoni yake katika mahojiano maalum na Idara ya Habari – MAELEZO, Mbunge wa Kaliua (CUF), Mhe. Magdalena Sakaya amesema bajeti hii ni nzuri kwani imeondoa tozo na ushuru ambavyo vilikuwa vikiwakera wananchi zikiwemo za taulo za akina mama na mabinti.

Mbunge huyo ameungamkono bajeti hiyo kwa kuishukuru Serikali kwa kujenga miradi mikubwa ya kuboresha miundombinu ukiwemo mradi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (Standard Gauge).

“Kwa kweli naipongeza Serikali kwa kujenga miundombinu ya reli na barabara kwani ujenzi wa uchumi wa viwanda bila miundombinu bora haiwezekani, ujenzi wa mradi mkubwa wa umeme wa Stiegler’s Gorge unaonyesha dhahiri jinsi Serikali ilivyo makini kwenye utendaji wake”, alisema Sakaya.

Naye Mbunge wa Pangani, Mhe. Jumaa Aweso katika mahojiano hayo amesema kuwa anampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kusimamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya miundombinu ya reli, maji na barabara kwani itasaidia juhudi za Serikali za ujenzi wa uchumi unaotegemea viwanda.

Aweso amesema Serikali inapojenga barabara na kuimarisha miundombinu ya maji itasaidia kuboresha kilimo hasa cha umwagiliaji kwani kilimo kitaweza kuwa chenye tija badala kilimo cha kizamani cha kutegemea hali ya hewa.

“Niseme wazi bajeti hii ni nzuri sana kwani inagusa maisha ya wananchi kwani imewaondolea kero za muda mrefu na itawafanya waweze kuongeza vipato kutokana na kuwekwa mazingira mazuri ya uwekezaji”, alisema Aweso.

Kwa upande wake, Mbunge wa Mvomero, Mhe. Suleiman Ahmed Sadiq amesema bajeti hii ni nzuri kwani imebuni vyanzo vipya vya mapato badala ya vilivyozoeleka vya kuongeza ushuru kwenye sigara, bia na soda.

Mhe. Sadiq amesema serikali imefanya vizuri kwa kupunguza kodi kwenye viwanda vya kutengeneza bidha a za ngozi ili kuchochea uwekezaji katika viwanda vya aina hiyo nchini.

Mbunge huyo amependekeza kuwa ushuru upunguzwe pia kwenye zana za kilimo ili kilimo kiweze kuwa cha kisasa na chenye tija.
Akitoa maoni yake kuhusu bajeti ya Serikali, Mbunge wa Njombe Mjini, Mhe. Edward Franz Mwalongo kuwa bajeti imekaa vizuri kwani inajenga uchumi imera kutokana na kujenga miundombinu imara ikiwemo ya Standard Gauge na ule wa umeme wa Stiegler’s Gorge.

Mwalongo amesema kuwa miundombinu bora itasaidia kutoa mazao shambani hadi sokoni na hivyo kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
Wabunge wanaendelea kuchangia bajeti kuu ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2018/19 kama livyowasilishwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango.


No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages