LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 14, 2018

BIL 23.061 KUTUMIKA KWENYE MATENGENEZO YA BARABARA PWANI 2018/2019

Mbunge wa jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka akiomba ufafanuzi juu ya ujenzi wa baadhi ya miundombinu ya barabara ,katika kikao cha bodi ya barabara Mkoani Pwani 
 Meneja wa wakala wa barabara Tanzania (TANROADS) Mkoani Pwani ,mhandisi Yudas Msangi akizungumza jambo ofisini kwake ,kuhusiana na masuala ya barabara Mkoani hapo
Mkuu wa Mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo,akizungumza jambo katika kikao cha bodi ya barabara Mkoani humo.(picha na Mwamvua Mwinyi)

Na Mwamvua Mwinyi,Pwani
KIASI cha sh. bilioni 23.061 zimepangwa kutumika kutoka mfuko wa barabara kwa ajili ya miradi ya matengenezo mbalimbali ya barabara ,mkoani Pwani, katika kipindi cha mwaka 2018/2019 .
Aidha katika kipindi hicho kiasi cha shilingi bilioni 10.4 zimepangwa kutumika kwa ajili ya matengenezo ya kilometa 518 za barabara kuu madaraja madogo 23 na makubwa mawili.
Hayo yamesemwa mjini Kibaha na meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani, Mhandisi Yudas Msangi wakati wa kikao cha bodi ya barabara ya mkoa huo.

Pamoja na hayo ,alisema kiasi cha shilingi bilioni 14 zitatumika kutengeneza barabara zinazounganisha maeneo muhimu ya kiuchumi ili kurahisisha mawasiliano kwenye maeneo hayo.
Hata hivyo ,Msangi alielezea shilingi bilioni 12.5 zitatumika kwenye matengenezo ya barabara za mkoa huo .
"Matengenezo ya kawaida lami kilometa 501.7 yametengewa shilingi bilioni 3.1, matengenezo maalumu lami kilometa 15.6 yametengewa kiasi cha shilingi bilioni 7 huku matengenezo ya sehemu korofi 0.7 kilometa yametengewa kiasi cha shilingi milioni 57.9,”alifafanua Msangi.
Alibainisha matengenezo madogomadogo ya madaraja 23 yametengewa kiasi cha shilingi milioni 74 na matengenezo makubwa ya madaraja mawili yametenegewa kiasi cha shilingi milioni 200.4.
Nae mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo ,alisema katika kuelekea kwenye ukanda wa viwanda ,ni lazima miundombinu ya barabara iboreshwe na kujengwa ili kuvutia wawekezaji.
Aliitaka Tanroads kutekeleza miradi hiyo kama ilivyoomba ili kutatua changamoto ya miundombinu ya barabara.
Ndikilo ,aliwaasa pia wananchi kulinda na kuacha kuharibu alama zinazowekwa barabarani .
Wakati huo huo mbunge wa Kibaha Mjini Silvestry Koka ,aliomba ufafanuzi juu ya ujenzi wa barabara ya kutoka Kwamatias hd Nyumbu.
Meneja wa TANROADs Pwani ,alimtoa hofu Koka kuwa barabara hiyo itajengwa mita 300 kwa mil.200.9 na ujenzi utaanza wakati wowote kuanzia sasa.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages