LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 27, 2018

NEC YATOA MAAMUZI RUFAA MGOMBEA UBUNGE NA RUFAA 5 ZA WAGOMBEA UDIWANI

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji (R) Semistocles Kaijage (katikati) akieleza jambo wakati wa Kikao cha Tume kilichokaa Ijumaa Januari 26, 2018 kujadili mambo mbalimbali yanayohusu Uchaguzi Mdogo unaofanyika Februari 17, 2018.Kulia kwake ni Makamu Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mkuu Mst. wa Zanzibar, Hamid Mahmoud Hamid na kushoto kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa Uchaguzi Hamis Mkunga na wajumbe wengine wa kikao cha Tume.Picha na Daniel Kasokola-NEC


Kwa kuzingatia masharti ya Kifungu cha 40(6) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, ikisomwa pamoja na Kanuni za 34 na 35 za Kanuni za Uchaguzi wa Rais na Wabunge za mwaka 2015, Tume ilipokea Rufaa moja (1) kutoka kwa Mgombea Ubunge Jimbo la Kinondoni kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF) akipinga maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo kuhusu pingamizi alilomuwekea Mgombea wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Aidha, kwa mujibu wa masharti ya kifungu cha 44 (5) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292, ikisomwa pamoja na Kanuni za 28 na 29 za Kanuni za Serikali za Mitaa (Uchaguzi wa Madiwani) za mwaka 2015, Tume ilipokea Rufaa tano (5) za Wagombea Udiwani kutoka katika Kata ya Isamilo – Halmashauri ya Jiji la Mwanza, wakipinga Maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo. Rufaa tatu (3) ni za wagombea walioondolewa kwenye kugombea ili warejeshwe na Rufaa mbili (2) zinaomba Tume itengue uteuzi wa mgombea Udiwani aliyeteuliwa katika Kata hiyo.

Katika kikao chake cha kawaida kilichofanyika tarehe 26 Januari 2018 siku ya Ijumaa, Tume ilipitia Rufaa hizo na kuamua kama ifuatavyo:

Mosi, kuhusu Rufaa ya Mgombea Ubunge, Tume imekubaliana na maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi na hivyo Mgombea aliyekatiwa Rufaa wa CHADEMA anaendelea kuwa mgombea wa Ubunge Jimbo la Kinondoni.

Pili, kuhusu Rufaa za Wagombea Udiwani Kata ya Isamilo katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza, kupinga kuondolewa kugombea Udiwani katika Kata hiyo, Tume imewarejesha kuwa Wagombea Udiwani wawili wa vyama vya CHADEMA na CUF.

Tatu, Tume imekubaliana na maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi ya kumuondoa katika orodha ya wagombea Udiwani mgombea wa Chama cha UDP. Hivyo hatakuwa mgombea katika kata hiyo

Nne, Tume imekataa rufaa mbili zilizokuwa zinapinga uteuzi wa mgombea wa CCM aliyeteuliwa katika Kata hiyo na hivyo, mgombea wa CCM anaendelea kugombea Udiwani katika kata husika.

Taarifa rasmi za maamuzi ya Tume zimetumwa kwa Wasimamizi wa Uchaguzi ili wawapatie wahusika maamuzi hayo.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages