LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jun 12, 2018

CHINA YAIOMBA TANZANIA NA CCM KUWA MWENYEJI WA MKUTANO WA KIDUNIA WA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeombwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa kidunia wa viongozi wa vyama vya kisiasa, maombi haya yamewasilishwa na Balozi wa China nchini Tanzania Bi. Wang Ke alipotembelea Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM Lumumba kuonana na Ndg. Bashiru Ally Kakurwa, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Balozi Wang Ke amefika Ofisi Ndogo za CCM kumletea Ndg. Bashiru Kakurwa ujumbe wa salamu za pongezi kwa kuteuliwa na Ndg. John Pombe Joseph Magufuli, Mwenyekiti wa CCM na kwa kauli moja kuchaguliwa na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kuwa Katibu Mkuu wa CCM.

Katika salamu zake Balozi Wang Ke ameeleza China na Chama Cha Kikomunisti cha China (CPC) kinampongeza Ndg. Bashiru na kwamba wako tayari kushirikiana naye katika masuala mbalimbali kama sehemu ya mahusiano ya muda mrefu kati ya Tanzania na China na vyama vya CCM na CPC. Aidha, Balozi Wang ametumia mkutano huo kuwasilisha ombi la China kwa Chama Cha Mapinduzi kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kidunia wa Viongozi wa Vyama vya Siasa ambao kwa mara ya kwanza unafanyika barani Afrika na unaotarajiwa kufanyika mwezi wa Julai 2018.

Chama Cha Kikomunisti cha China (CPC) kimeichagua Tanzania na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa mwenyeji wa mkutano huu mkubwa na wa kihistoria “CPC Dialogue with World Political Leaders in Africa”. Mkutano huu wa kidunia unabeba kauli mbiu isemayo nadharia na vitendo katika kutambua njia sahihi za maendeleo ambazo ni endelevu na halisia kwa nchi zetu. Tunayo furaha na heshima kubwa kuwa na mkutano huu mkubwa Afrika na Tanzania kama sehemu ya Mpango wa kuiunganisha dunia kwa barabara na usafiri wa maji ulioasisiwa na Ndg. Xi Jinping Katibu Mkuu wa CPC na Rais wa China amesema Bi. Wang Ke.

Akipokea salamu hizo za pongezi Ndg. Bashiru Ally amemhakikishia Balozi Wang kwamba Chama Cha Mapinduzi kitaendeleza mahusiano ya kidugu na ya kihistoria kati ya CCM na CPC na nchi zetu mbili.

Tunataka kujifunza zaidi kutoka China na hasa namna ya kujipanga kimkakati katika kushughulika na kuendeleza mapambano dhidi ya dhuluma na unyonyaji ili nchi yetu iinuke na kuleta manufaa makubwa kwa watu wetu wa Tanzania. Ndg. John Pombe Joseph Magufuli, Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anayo kazi ya kujenga uchumi utakaowezesha kujitegemea, uchumi wa kitaifa, uchumi utakaowaondoa watanzania kutoka katika maisha ya umasikini kama China na kwa msingi huu kama Chama na Ilani tumejitambulisha kuhudumia wanyonge na kushughulika na shida za watu amesema Ndg. Bashiru Ally Kakurwa Katibu Mkuu wa CCM

Huu ni mwendelezo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuimarisha mahusiano ya ndani na ya nje katika eneo la siasa, diplomasia na uchumi.

Imetolewa na,
  
IDARA YA ITIKADI NA UENEZI
CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM)
OND LUMUMBA 

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages