HABARI MPYA

Your Ad Spot

May 13, 2016

CCM YAKANUSHA UTAPELI




Na Mwandishi Wetu, Zanzibar.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimelaani vikali tabia ya baadhi ya watu wanaotumia vibaya jina la Chama hicho kuwatapeli wananchi kutoa fedha ili wapatiwe nafasi za ajira katika Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) jambo ambalo sio sahihi.

Kimewataka wafuasi wa Chama hicho na wananchi kwa ujumla kuacha tabia ya kuwaaminisha watu  kwamba CCM inatoa nafasi mbali mbali za ajira kwani kufanya hivyo ni kuwagombanisha viongozi na wananchi wao.

Akitoa taarifa kwa Vyombo vya Habari, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Ndugu Vuai Ali Vuai alisema Chama hicho hakihusiki na utoaji wa ajira ya aina yoyote, hivyo watu wanasambaza utapeli huo kwa njia ya simu na mitandao ya kijamii lengo lao ni kuchafua taswira njema ya chama hicho.

Akifafanua zaidi Ndugu Vuai amesema suala la ajira katika taasisi za kiserikali na binafsi zinazolewa kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa hasa baada ya kutolewa matangazo maalum kulinga na nafasi za ajira zilizopo na sio kutumia simu za mkononi kuwapigia watu ili waweze kutoa fedha kwa ajili ya kuwapatiwa ajira hizo.

“Nimepigiwa simu nyingi na baadhi ya watu wangu wa karibu wakiniuliza juu ya taarifa za Chama kuwa kuuza nafasi za ajira, taarifa ambazo nimezipokea kwa mshangao mkubwa kwani ndani ya chama chetu hakuna utaratibu huo” na kuongeza kusema kwamba “nawataka wananchi kuwa macho na makini na matapeli wanaotumia hila tofauti kuwaadaa watu kwa nia ya kujipatia fedha kwa njia za 
udanganyifu”. Alisisitiza Vuai.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Zanzibar, alitoa wito kwa wananchi kuwa makini na matapeli hao na mtu yeyote atakayepigiwa simu na kuambiwa atoe kima chochote cha fedha kwa lengo la kupatiwa ajira na CCM asikubali kufanya hivyo na badala yake atoe taarifa haraka katika vyombo vya dola, ili sheria ichuke mkondo wake.

Aliwasihi wananchi kuendelea kuamini  kwamba CCM ni Chama kilichokomaa kisiasa na uzoefu mkubwa wa kusimamia demokrasia ya kweli, usawa, haki, utawala bora, a hivyo hakiwezi kujihusisha na vitendo viovu kwa jamii.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM alisisitiza kua; suala la ajira za JWTZ, Idara Maalum za SMZ na zile za Taasisi nyengine za seriikali, zote hizo zinatolewa kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizowekwa na Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW).
Alisema kuwa haiwezekani hata kidogo Chama hicho (CCM) kitowe ajira na kuongeza kuwa taarifa hizo zinazosambazwa na watu ni za kitapeli na zinalenga kuchafua jina la Naibu Katibu Mkuu huyo pamoja na CCM kwa jumla.
Aliwaomba wananchi wazipuuze taarifa hizo na wawe macho na utapeli wa aina hiyo uliozagaa Zanzibar na maeneo mengine nchini, kwani unafanywa na wapinga maendeleo ya CCM na Taifa kwa jumla.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages