LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Apr 1, 2016

LUHWAVI: WATUMISHI WA CHAMA CHACHU YA CCM KUNG'ARA KATIKA JAMII

Na Bashir Nkoromo, Njombe
Watumishi wa Chama ni sehemu muhimu inayokifanya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuendelea kuwa bora na imara kwa kuwa ndiyo jiko la kubuni na kuandaa taswira ya muonekano wa Chama katika jamii.

Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara) Rajabu Luhwavi wakati akizungumza na watumishi wa Chama Cha Mapinduzi kutoka wilaya za mkoa wa Njombe na Ruvuma, jana, akiwa katika ziara ya kikazi katika mkoa huo kuzungumza na kusikiliza changamoto na kero zinazowakabili watumishi wa Chama. 

Alisema, ni kutokana na kutambua umuhimu wa watumishi hao ndiyo sababu Chama Cha Mapinduzi kinafanya kila jitihada kuhakikisha kinakutana nao ili kujua mazigira walioyomo na changamoto na kero zinazowakabili ili kuweza kutafuta njia za kuzitatua kwa kadri inavyowezekana.

"Unajua mimi ndiyo nasimamia utumishi katika chama, kazi zingine zote zinazonihusu naweza kuzifanya kupitia mafaili nikiwa ofisini, lakini hili la kuhusu mazingira na hali za watumishi ambalo pia linanihusu siweze kulifanya nikiwa ofisini, ndiyo sababu nimeamua kufanya ziara hizi, ili niwasilikilize kero na changamoto zinazowakabili tukiwa pamoja", alisema Luhwavi.

Alisema, anatambua zipo kero na changamoto kadhaa miongoni mwa wafanyakazi, lakini siyo rahisi kujua ukumbwa na namna zilivyo bila kutumia njia hiyo ya kuzungmza na watumishi katika maeneo waliko.

Hata hivyo Luhwavi alisema licha ya kuwepo kero na changamoto lakini ni lazima kila mfanyakazi ndani ya Chama kuhakikisha anafanyakazi kwa weledi, hekima na maarifa ili kuleta tija inayokusudiwa, kwa kuwa bila kufanya hivyo matarajio yanayotakiwa kukifikisha Chama kunakotakiwa hayatafikiwa.

Aliwataka wafanyakazi kuendana na kasi ya mabadiliko ambayo Chama kimejipangia kuyafanya ili kuendana na wakati wa sasa, akionya kwamba kama kuna mfanyakazi ambaye atashindwa kumudu kwendana na kasi hiyo atawekwa pembeni na kuendelea na wale wanaoimudu.

Luhwavi aliwataka watumishi wa Chama kuwa mstari wa mbele katika kumuunga mkono, Rais Dk. John Magufuli katika jitihada zake za kuleta mabadiliko ya kiuchumi wa taifa na kijamii, ambayo ameanza kuitekeleza ikiwemo 'kupasua majibu' kwa kuwawajibisha watendaji wabadhirifu na wasiowajibika katika dhamana au kazi walizokabidhiwa na umma.

"Kumbukeni upasuaji huu wa majipu unaofanywa na Rais wetu, Dk. JPM (John Pombe Magufuli), ni utekelezaji wa yale yaliyopitishwa na Chama Cha Mapinduzi na kuyaweka katika ilani yake ya Uchaguzi wa 2015-2020), sasa itashangaza sana kuona wakati Rais anayetokana na Chama chako anafanya utekelezaji wewe badala ya kumuunga mkono unajiweka pembeni, hii siyo sahihi", alisema Luhwavi.

Alisema, ni lazima watumishi na wanachama wa CCM kwa jumla kuhakikisha kila mmoja kwa nafasi yake anamuunga mkono Rais Magufuli katika kazi hiyo kubwa na ngumu anayoifanya kuhakikisha taifa la Tanzania lipata mabadiliko ya dhahiri kivitendo kwa sababu bila kufanya hivyo hayataweza kupatikana mafanikio ya haraka katika kazi hiyo ya rais.

Mapema, akimkaribisha Naibu Katibu Mkuu kuzunguza na watumishi hao, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Njombe Deo Sanga, maarufu kwa jina la 'Jah People', aliwataka wafanyakazi hao kuzungumza bila woga kero na changamoto zinazowakabili akisema kikao hicho ndiyo mahala mwafaka badala ya kukaa kimya na kwenda kulalamika barabarani.

Katika kikao hicho kila mtumishi aliyekuwepo katika kikao hicho alipewa nafasi ya kueleza ya moyoni mwake, ambapo katika kueleza kero zao, wengi waliomba Chama kuongeza mishahara na maslahi mengine kwa wafanyakazi wa Chama ili kuwa kichocheo cha kuwafanya wachapekazi kwa bidii zaidi.

Baadaye Naibu Katibu Mkuu, alizungumza na Makatibu wa matawi na Kata wa CCM kutoka katika wilaya ya Njombe,kikaoambacho kilifanyika katika Ofisi ya CCM mkoa wa Njombe na kuhudhuriwa na wajumbe wengi.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages