LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Apr 21, 2013

KINANA AICHAMBUA CHADEMA

*Asema viongozi wake wamekubuhu wa ubinafsi
*Wanajali maslahi binafsi ya Chama chao badala ya Watanzania
*Awatakja Watanzania kuwapuuza
Kinana akihutubia mjini Morogoro leo.Picha: Bashir Nkoromo
NA BASHIR NKOROMO, MOROGORO
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana ameisasambua Chadema na kusema ni chama ambacho daima kimekuwa kikiweka mbele maslahi yake binafsi kuliko ya Watanzania.

Amesema viongozi wa chama hicho wamekubuhu kwa udikteta kiasi cha kujiona wao ndio wanajua kila jambo kuliko watu wengine hata mwenzao wa chama cha upinzani ikitokea ana mawazo  au msimamo wasioutaka au ameipongeza serikali kwao huonekana ni msaliti na kibaraka wa CCM.

Akihutubia leo mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika jana mjini hapa,Kinana, alisema kuwa Chadema ni balaa kwa nchi naa watu kwani viongozi wake wamekuwa ni watu wa kuhubiri machafuko badala ya mshikamano uliozoeleka Tanzania.

Alisema kutokana na umangimeza wao sasa Chadema kimeanza kuigawa nchi kwa kutumia sera ya ukanda licha ya kwamba sera hiyoi ni kinyume cha katiba ya nchi na watu wake.

"Ninapenda leo niwaelezeni ndugu Watanzania Chadema ilivyojawa na ubinafsi, wamekuwa wakiwakukusanya Watanzania na kuwagawa kwa sera yao ya majimbo. hili si mara ya kwanza maana katika kipindi cha siku za hivi karubuni walitangaza wazi kuigawa nchi kwa kutaka
kujitenga kanda ya Kaskazini eti ili iwe chini ya utawala wao", alisema Kinana.

Kinana alisema CCM kama chama kilichoingia mkataba na Watanzania haiwezi katu kukaa kimya na kuona hali hii ikitokea, kila mara tumekuwa tukihubiri amani na mshakamano lakini Chadema hili limewashinda jambo ambalo alisema ni dalili kwamba viongozi wa Chadema wameingia katika siasa kwa malengo yao binafsi.

"CCM itaendelea kusema ukweli kwa kila jambo na wala haitaficha hata likiwa siyo la kufurahisha wanachama wake ili mradi ni la kweli, tofauti na  hawa Chadema, lazima Watanzania muwe makini nao kutokana na aina ya siasa na matendo yao wanayojinasibvu nayo" alisema Kinana.

Vurugu za Chadema
Kinana alisema kuwa Chadema wamekuwa ni watu wa maajabu na vurugu kubwa nchini, na katika hilo alitoa mfano ya mambo ambayo wanayafanya bungeni.

"Chadema kazi yao ni vurugu tu, utadhani wao ndio wamekuwa kambi ya upinzani wa kwanza bungeni katika nchi  hii. Walikuwepo wapinzani  kabla yao lakini kama CUF na Kina Mrema (Augustine Mrema) enzi za NCCR Mageuzi lakini hamkupara kushuhudia vituko kama

hawa Chadema ambao wanajiona wao ndio kila kitu. Wanatoa vitisho kila siku kwa Serikali hata kumtukana mkuu wa Nchi bila kujali kwamba ni kiongozi ambaye amefika pele kwa kuchaguliwa na idadi kubwa ya Watanzania", alisema.

"Wanabeza wapinzani wengine , wakiona mpinzani anapongeza kazi iliyofanywa na CCM wanaanza kumshambulia.Hakuna anayejua zadi ya Chadema .Wanamtukana Rais, wanaushambulia usalama wa Taifa, wanashambulia vyombo vya usalama,"alisema Kinana

"Hawa jamaa ni watu wa ajabu sana, kila kitu wanajua wao wengine hawajui.Wakigombana katika chama chao utasikia kuna mkono wa CCM. Sijui ni watu wa aina gani , wanafanya mambo ya ajabu sana kiasi cha kushangaza,"alisema.

Kinana alitoa ushauri kwa Chadema kuwa na uwezo wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo yao kuliko kutumia muda wao mwingi kila jambo ambalo linakwenda kombo kunyoosha vidole kwa CCM.

"CCM tuna changamoto zetu nyingi, lakini tunatatua matatizo yetu wenyewe hatupotayari.Tuna makundi ndani ya chama lakini hayo ndio mambo ya siasa,"alisisitiza.

Mchakato wa Katiba mpya
Kinana alisema pamoja na kazi nzuri ambayo imefanywa katika mchakato wa Katiba mpya, kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni ametoa hotuba yake ambayo inaonesha wazi hakuna ambacho kimefanyika katika mchakato huo.

Alisema kuwa kiongozi wa kambi ya upinzani Freeman Mbowe akiwa bunge ametumia muda wake mwingi kuzungumzia mchakato wa katiba mpya na kubwa katika hotuba yake kuwa haufai.

"Simsingizii kiongozi wa Kambi ya upinzani bungeni, ndani ya hotuba yake ameeleza wazi kuwa waliopewa dhamana ya kukusanya maoni ya Katiba mpya hawana ujuzi.Hii si kweli, waliopewa dhamana hiyo ni watu ambao wanaifanya kazi hiyo kwa uadilifu,"alisema.

Alisema Chadema ni watu binafsi ambao wao wametawaliwa na uroho mkubwa na wao kazi ni kuangalia maslahi zaidi na ni si maslahi ya nchi.

Ziara yake Morogoro
Kinana alisema kuwa ziara yake amejifunza mamb mengi lakini kubwa na msingi ambalo lipo kwa chama hicho kitahakikisha kinatafuta ufumbuzi wa matatizo ya wananchi na hasa migogoro ya ardhi, mipaka na huduma za jamii ambazo nazo ni changamoto kubwa kwa maeneo mbalimbali.

"Ziara yangu na viongozi wengine wa chama chetu ambayo tuimefanya katika wilaya zote za Morogoro tumeona changamoto nyingi.Tumetafuta ufumbuzi wa matatizo lakini mengine yanapatiwa ufumbuzi baada ya kukaa na viongozi wa ngazi mbalimbali wa chama na kisha kutoa maagizo kwa Serikali kutekeleza,"alisema.

Agizo kwa wabunge CCM
Katibu Mkuu huyo wa CCM, alitumia nafasi hiyo kwa kuwataka wabunge wa CCM kutembea kifua mbele kwani chama chao kinafanya kazi kubwa lakini aliwataka wawe makini na Chadema na kuwataka kutowasikiliza kwani sasa imetosha.

Alisema Chadema wamekuwa wakisikiliza muda mrefu ndani ya Bunge na kuna wakati wabunge wa CCM walichukia baada ya Rais Jakaya Kikwete kukubali kukutana nao kujadili mchakato wa Katiba Mpya.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages