LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Apr 4, 2020

WABUNGE WATOA YA MOYONI JANGA LA CORONA, PROF. TIBAIJUKA ATAKA TIBA MBADALA ITUMIKE


Na Said Mwishehe, Michuzi TV

WABUNGE wameendelea kutoa maoni na ushauri kwa Serikali kuhusu hatua inaweza kuzichukua kwa ajili ya kukabiliana na ugonjwa wa COVID-19(Corona) huku Mbunge wa Muleba Kusini Profesa Anna  Tibajuka akitaka tiba mbadala nayo itumike kwenye kukabiliana na ugonjwa huo.

Wakizungumza Bungeni Mjini Dodoma kwa nyakati tofauti leo Aprili 3 mwaka 2020, wabunge ambao wamepata nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu, wametumia nafasi hiyo kutoa maoni yao kuhusu janga la Corona ambalo limeleta madhara makubwa ulimwenguni kote.

Kwa mujibu wa wabunge hao wamesema kwanza Watanzania hadi walipofikia sasa tangu kuanza kwa ugonjwa huo wanayo sababu ya akumshukuru Mungu kwani amewalinda sana na ugonjwa huo ambapo idadi ya walioambukizwa Corona ni watu 20.

Mbunge Prof. Tibaijuka amesema ugonjwa wa Corona umeleta madhara makubwa katika nchi mbalimbali na iwapo kasi ya maambukizi itakuwa kubwa nchini kwetu na athari zake zinaweza kuwa mbaya zaidi.Hivyo badala ya kuangalia tu plani A ni vema sasa ikaangaliwa na plani B kwa maana ya tiba mbadala.

"Kuna ushauri ambao unatolewa na watalaam wa afya, wakituhimiza kunawa maji kwa mikono na sabuni, lakini tunafahamu wakati tunahamasisha wananchi kunawa maji kuna maeneo hawana maji.Hivyo tuangalie na upande wa tiba mbadala, wengine tumekaa vijijini na wazee wetu walikuwa wanatumia tiba mbadala kwa ajili ya kutibu magonjwa na watu walipona.

"Nilikua naangalia takwimu katika nchi ya Ghana ambako kuna wagonjwa 35 wamepona Corona na dawa ambayo wametumia ni mwarobaini.Hivyo nasi tunaweza kuangalia tiba mbadala kama njia nyingine ya kupambana na Corona, tunayo makabilia mengi nchini na kila moja linaweza kusaidia namna ya kupata tiba,"amesema Profesa Tibaijuka.

Akifafanua zaidi kuhusu Corona,amesema historia inaonesha ni ugonjwa ambao huwa unatokea kila baada ya miaka 100 huku akisisitiza iko haja ya kuwa na njia mbadala ya kutibu ugonjwa huo."Mungu  akitusaidia na kuvuka salama kwenye hili lazima tuangalie sasa na tiba mbadala.Namshukuru Rais kwa kuhimiza watu kuendelea kufanya sala na ukweli Mungu anatupenda Watanzania."

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Muheza mkoani Tanga Balozi Adadi Rajabu ameliambia Bunge pamoja na jitihada zinazochukuliwa na Serikali inazichukua kukabiliana na janga la Corona ambapo ameshauri kuwe na bajeti ya fedha ambayo itatumika kukabiliana na janga la ugonjwa huo.

"Ni vizuri Serikali ikatenga fungu maalum la fedha, hakuna sababu ya kusubiri hali iwe mbaya kwani tutashindwa kuzuia Corona. Najua kuna Kamati imeundwa lakini ni vema fedha ni zikatengwa na  nashauri wabunge tuchangie fedha kwa ajili ya kukabiliana na janga la Corona,"amesema Balozi Rajabu.

Akizungumza baada ya maoni na ushauri wa wabunge Spika Job Ndugai amesema kuna kila sababu ya mkono wa wabunge kuonekana kwenye janga hilo la Corona kwa maana ya kuchanga fedha."Tutaangalia namna ya kufanya ili na wabunge nao wachangie fedha badala ya kuonge maneno matupu."

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages