LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 9, 2018

MOI YAWAFANYIA KIPO CHA UMRI WACHEZAJI WA CECAFA 2018


NA KHAMISI MUSSA


TAASISI ya Tiba na Mifupa (MOI),imesema kuwa inatarajia kukamilisha zoezi la upimaji wa vijana wenye umri wa miaka 17 wanaoshiriki katika michuano ya kombe la Cecafa 2018 leo ambapo michuano hiyo inatarajia kuanza kurindima Agosti 11,2018.

Akizungumza na CCM Blog jana katika Taasisi hiyo, Ofisa Uhusiano wa MOI Patrick Mvungi alisema kuwa timu za Taifa ambazo zimewisha peleka vijana hao ni pamoja na Tanzania Serengeti boy, Burundi, Sudan, Djibout na Ethiopia.

Mvungi aliongeza kuwa awali Shirikisho la soka barani afrika (CAF),lilifika katika taasisi hiyo na kufanya tathimini ya vifaa pamoja na wataalamu ambapo waliona MOI imekidhi viwango vya Kimataifa vya Shirika la Afya Duniani (WHO).

Alisema kuwa katika upimaji huo wanatumia kipimo kinachoitwa MRI ambacho kinabaini umri halisi na kwamba vijana hao watapimwa mkono wa kushoto kwa kuangalia mifupa ya kiganja na kuweza kujua umri halisi.

“Suala la matokeo ya vipimo ni la CAF sisi hatuhusiki kazi yetu ni kuwapima tu wenye maamuzi ya kusema mchezaji aliyedanganya umri ni CAF,”alisema Mvungi.



Mkurugenzi Mtendaji wa MOI Dkt. Respicious Boniface alisema ni heshma kubwa kwa Taasisi kupewa fursa ya kupima umri wa wanamichezo hao ambao wanatoka mataifa mbalimbali na Tanzania ikiwemo.

 “Taasisi yetu ina vifaa vya kisasa kama hivi vinavyotumika kupima umri kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ya awamu ya 5 inayoongozwa na Mh Dkt. John Pombe Magufuli, kwakweli tunamshukuru sana Mh Rais kwa uwekezaji huu” Alisema Dkt. Boniface

Dkt. Boniface alisema changamoto ya kudanganya umri kwa wanamichezo inaweza kumalizika kabisa kwani kabla ya hapo kumekuwa na udanganyifu mkubwa wa umri hususani kwenye bara la Afrika.

Aidha, Mkurugenzi wa Tiba wa MOI Dk. Samuel Swai alisema zoezi la upimaji wa umri linaendeshwa na madaktari bingwa wa MOI kwa usimaizi wa maafisa kutoka shirikisho la soka  barani Afrika (CAF) na kwa siku ya kwanza zaidi ya wachezaji 40 walipimwa.

“Tunashukuru kwa kupewa heshima kubwa miongoni mwa hospitali nyingi zilizokaguliwa hapa nchini, naamini umahiri wetu na vifaa vya kisasa ndio siri ya mafanikio, kwa hili tutahakikisha tunafanya kazi kwa uaminifu mkubwa ili kulinda heshima ya Taasisi na nchi yetu,”alisema Dk. Swai.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages