LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 5, 2018

MBUNGE ATOA UFADHILI WA MASOMO KWA WANAFUNZI WA JIMBO LAKE MKOANI SINGIDA


Na Dotto Mwaibale, Singida

MBUNGE wa Jimbo la Singida Magharibi, Mheshimiwa Elibariki Kingu (pichani), ametoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wote wa kidato cha tano na sita katika Jimbo lake ambao wameenda kusoma katika shule mbalimbali nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Kingu alisema wanafunzi hao wamepata ufadhili huo kupitia taasisi yake ya Kingu Scholarship Programe na kuwa tayari wamekwisha walipia ada zao.

"Nimeona ni vizuri wanafunzi wote waliopo katika jimbo langu ambao wanaenda kuendelea na masomo yao ya kidato cha tano na sita niwalipie ada kwani hilo ni moja ya jukumu langu kama mbunge wao" alisema Kingu.

Alisema katika suala la kuinua elimu ni jukumu la kila mmoja wetu na si kuiachia serikali pekee ambayo inamaeneo mengi ya kushughulikia ndio maana aliwiwa kuwasaidia wanafunzi hao.

Alisema watoto wengi wanauwezo wa kimasomo lakini baadhi yao wanashindwa kuendelea na masomo kutokana na changamoto mbalimbali hivyo wakiachwa bila ya kusaidiwa taifa litakosa wataalamu siku za usoni.

Kingu alisema ameanzisha taasisi hiyo kwa lengo la kuwasaidia watoto wa wakulima ambao watafaulu kidato cha nne na kupata nafasi shule za serikali hapa nchini kuwa watalipa ada zao hadi hapo watakapo maliza masomo yao kwani elimu ndio silaha pekee ya kumkomboa mkulima na mfugaji.

Alitaja orodha ya baadhi ya wanafunzi waliopata ufadhili huo pamoja na shule wanazokwenda kusoma kuwa ni Magret Emanuel ambaye anakwenda Sekondari ya Monduli, Raymond Yahya (Same Sekondari), Aisha Jumanne (Loleza), Mariam Rashid (Ifakara) na Petro Shija, Tarime.

Kingu aliwataja wanafunzi wengine kuwa ni Samwel Suku anayekwenda Iyumbu Sekondari, Faudhia Hamisi (Urambo), Yakini Ezekia (Rungwe), Latifa Rashidi (Igowole), Baraka Ibrahim (Aman Abed), Bertha Emmanuel (Bungu), Binzura Shabani (Maweni) na John Lameck (Ilboru)

Wanafunzi wengine ni Haruna Juma anayekwenda Bihawana Sekondari, Nyamata John (Isimila), Debora Elibariki (Iyumbu), Shamimu Ali (Anaghwai), Lambo Mahona (Loleza) na David Khalfan anayekwenda Sekondari ya Tukuyu TTC. 

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages