LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jul 3, 2018

RAIA 18 WAUAWA KATIKA MACHAFUKO MAPYA SUDAN KUSINI

Watu wasiopungua 18 wameuawa katika machafuko mapya yaliyozuka nchini Sudan Kusini, baada ya kukiukwa makubaliano mapya ya amani yaliyosainiwa siku chache zilizopita katika nchi jirani ya Sudan.
Pande hasimu katika mgogoro wa nchi hiyo zinarushiana lawama juu ya vifo hivyo vya raia wasio na hatia katika jimbo la Upper Nile, kaskazini mashariki mwa nchi.
Lul Ruai Koang, msemaji wa Jeshi la Serikali nchini humo SPLA  amesema genge la waasi ndilo lililovamia mji wa Maban jimboni Upper Nile, ambapo vikosi vya serikali vililazimika kuingilia kati. Amesema raia 18 waliuawa na waasi hao katika makabiliano hayo, wakiwemo raia watatu wa Ethiopia na wawili wa Sudan, mbali na wengine 44 kujeruhiwa.
Hata hivyo, Lam Paul Gabriel, naibu msemaji wa kikosi cha waasi cha SPLA-IO amesema wapiganaji wa genge hilo walishambuliwa vikali kwa mabomu na silaha nyingine nzito na askari wa serikali Jumapili iliyopita, huku akikanusha madai kuwa wao ndio walioua raia.
Riek Machar (kushoto), Rais Yoweri Museveni wa Uganda, mwenzake wa Sudan Omar Bashir na Salva Kiir, Khartoum
Jumamosi iliyopita, Moussa Faki Mahamat, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika AU akizungumza katika mkutano wa umoja huo mjini Nouakchott nchini Mauritania alisema kuwa, wakati umefika wa kuwachukulia hatua wahusika wanaochochea mgogoro nchini Sudan Kusini.
Aliyasema hayo baada ya mapatano ya hivi karibuni ya usitishaji vita nchini Sudan Kusini kukiukwa, masaa machache baada ya kuanza kutekelezwa huku pande zote mbili za serikali na upinzani zikirushiana lawama.
Pande hasimu ziliafiki Jumatano iliyopita kuhusu usitishaji vita wa kudumu baada ya mazungumzo kati ya mahasimu wawili wa kisiasa yaani Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini na makamu wake wa zamani, Riek Machar, katika mji mkuu wa Sudan, Khartoum. 

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages