LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jul 29, 2017

SERIKALI YAPONGEZWA KWA KUPUNGUZA UKATILI DHIDI YA WATU WENYE ULEMAVU WA NGOZI NCHINI

NA BUSHIR MATENDA- MAELEZO
Serikali ya Tanzania imepongezwa kwa jitihada zake za kukabiliana na mashambulizi dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albinism) ambazo zimepelekea kupungua kwa kiasi kikubwa cha vitendo hivyo vya kikatili dhidi yao.

Akiwasilisha Taarifa ya Utafiti wake, Mtaalamu wa Kujitegemea kuhusu kunufaika na haki za binadamu kwa watu wenye ulemavu wa ngozi, Mtaalamu wa kujitegemea Bi. Ikponwosa Ero amesema kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kushughulikia kadhia inayowapata watu wenye ulemavu wa ngozi.

“nimefurahishwa na taarifa ya kupungua kwa idadi ya mashambulizi yaliyoripotiwa na naipongeza Serikali ya Tanzania kutokana na juhudi zake  kushughulikia tatizo hilo” alieleza Mataalamu huyo.

Aliongeza kuwa hatua za Serikali za kukabiliana na vitendo vya ushirikina ambavyo ndio kichocheo kikubwa cha vitendo vya ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi hazina budi kuambatana na kutolewa elimu zaidi kwa jamii ili waache imani potofu dhidi ya matumizi ya viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi katika kupata utajiri.

Hata hivyo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa pamoja na kupungua kwa vitendo vya mashambulizi dhidi ya watu hao lakini bado watu wenye ulemavu wa ngozi wanaendelea kuishi kwa hofu kwa kuwa chimbuko la ukatili huo bado lipo.

“Watu wenye ulemavu wa ngozi pamoja na maswahiba mengine ya kimaisha kama umasikini na ukosefu wa elimu lakini bado wanaendelea kuishi kwa hofu hususan katika maeneo ya vijijini” alisema Bi Ero.

Bi. Ero, raia wa Nigeria, ambaye ni mmoja wa watalaamu wa haki za biandamu wa Umoja wa Mataifa, alieleza kutiwa moyo hali ya ushirikiano uliopo kati ya Serikali na wadau wengine wakiwemo Umoja wa Mataifa na Asasi za Kiraia hali ambayo imesaidia sana Tanzania kupata mafaniko kupunguza vitendo vya ukatili dhidi ya albino.  

“Ni faraja kubwa kuona Serikali inafanya kazi bega kwa bega na asasi za kiraia katika sekta ya elimu na afya, hasa katika kuwapatia vifaa vya kuonea pamoja na kuanzisha huduma za kliniki kwa magari ili kuzuia kansa ya ngozi” alibainisha Bi. Ero

Mtaalamu huyo ambaye aliwasili nchini tarehe 18 Julai, 2917 alibainisha kuwa akiwa nchini alipata fursa ya kutembelea mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Kigoma, Shinyanga na Mwanza ambako alionana na watu mbalimbali kutoka Serikalini, asasi za kiraia, watu walioathirika na vitendo dhidi ya maalbino pamoja na familia zao.

Katika utafiti huo ambao anatarajia kuuwasilisha katika Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa mwezi Machi mwakani, Bi Ero alieleza kuwa bado jitihada zaidi zinahitajika katika kuelimisha wananchi kuhusu hali ya watu wenye ulemavu wa ngozi ili waweze kuwakubali warudipo katika jamii baada ya kuishi kwenye kambi maalum ikiwemo watoto wanaoishi katika shule za bweni.

“Nina wasiwasi kuwa makambi hayo yaliyoanzishwa kwa muda yanaonekana kuwa sasa yamageuzwa kuwa makaazi ya kudumu kwa watu hao kwa kuwa bado jamii haijawakubali kwa hivyo wanasita kuwapokea” 

Nae Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini Alvaro Rodriguez ameishukuru Serikali ya Tanzania chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John pombe Magufuli kwa kumruhusu Mtaalamu huyo wa kujitegemea kuja kufanya tafiti  utafiti huo.

Alibaisha kuwa hatua hiyo ya Serikali inadhihirisha dhamira yake ya kushughulikia kwa dhati changamoto mbali mbali zinazowakabili watu wenye ulamavu wa ngozi nchini.

Bwana Rodriguez amepongeza jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali katika kuhakikisha watu wenye ulemavu wa ngozi wanakuwa salama muda wote katika jamii zao na jitihada endelevu ya kuboresha mambo muhimu kwa watu wenye ulemavu wa ngozi ikiwemo vifaa vya kuona, huduma bora ya Afya na kuwaendeleza katika elimu.

Bi.  Ero aliwasili nchini 2017 akifanya tathmini juu ya hali ya haki za binadamu kwa watu wenye ulemavu wa ngozi kwa kujizangatia jitihada zinazofanywa na Serikali na wadau mbalimbali kuboresha ustawi na haki zao.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages