LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Apr 27, 2017

DR. MABODI AWATAKA WANANCHI KUITUMIA HOTUBA YA DKT. MAGUFULI KAMA NYENZO

NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar   kimeunga mkono na kuipongeza hotuba iliyotolewa na  Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe  Magufuli katika sherehe za miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar jana Mjini  Dodoma.

Akizungumzia hotuba hiyo Naibu Katibu Mkuu wa CCM- Zanzibar,  Dkt. Abdalla Juma Saadala “ Mabodi”,  alisema imejaa dhamira na mikakati endelevu ya kuimarisha Muungano huo alioutaja kuwa ni chachu ya kumaliza wimbi la umaskini kwa wananchi.

Alieleza kwamba misimamo wa Rais Dkt. Magufuli kupitia hotuba hiyo umekuwa ni sehemu ya wananchi wa rika na kada tofauti kujifunza na kuelewa kwa kina historia halisi ya nchi hizo zilipotoka, zilipo na zinaelekea wapi katika ustawi wa Nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii.

 Dkt. Saadala alifafanua kwamba miongoni mwa mambo ya msingi yaliyosisitizwa na Dkt. Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, kwa kuwambia wananchi waweke kando itikadi za kisiasa na kidini badala yake wavae rasmi joho la uzalendo ili kuweka kinga ya kudumu ya muungano huo dhidi ya maadui.

 Aidha ameongeza kwamba mbali na hamasa hiyo pia ujumbe huo uliwataka viongozi wa Chama na Jumuiya, sekta binafsi na serikali pamoja na wananchi kwa ujumla kufanya kazi kwa bidii, kwa nia ya kuendeleza mambo mema yalioasisiwa kama urithi yakiwemo muungano wa serikali mbili  ili nchi hizo zijitawale kiuchumi.

“CCM na wananchi wapenda Amani na Utulivu wa nchi zetu kwa pamoja tunaunga mkono hotuba na matamko yaliyotolewa na Rais wetu mpendwa Dkt. Magufuli huko katika sherehe za za kutimiza miaka 53 tangu kuzaliwa kwa Muungano imekuwa ni shamba darasa la kutukumbusha wajibu wetu kama wananchi ili na sisi tutende haki kwa nchi zetu.”, alifafanua Dkt. Mabodi, na kuongeza kwamba kipimo cha uzalendo na utaifa ni kuweka mbele maslahi ya nchi na kujitenga na vitendo vinavyoweza kuchafua amani ya nchi.

Akizungumzia suala la maendeleo na mikakati ya kuimarisha uchumi wa  SMZ na SMT, Dkt. Mabodi alisema hotuba hiyo imeweka wazi kuwa mkakati wa maendeleo utakuwa ni endelevu kwa sekta za kiafya, kielimu, uvuvi, kilimo, ufugaji, miundombinu, utalii sambamba na kupigania falsafa ya Tanzania yenye viwanda.

Hata hivyo amepongeza suala la Rais huyo kuendeleza utamaduni wa kuthamini juhudi zilizofanywa na vyama vya ukombozi vya Tanzania Bara na Zanzibar vikiwemo ASP na TANU vilivyoongozwa na Hayati Mwl. Juliusi Kambarage Nyerere na Marehemu Abeid  Aman Karume na baadae vikaungana na kuzaliwa kwa CCM.

Naibu katibu Mkuu huyo alisema hotuba hiyo iliyowasilishwa kwa ufasaha na utulivu mkubwa na Rais huyo, hali iliyoashiria  thamani  na uzito wa  maudhui yake kwa  umma kupitia sherehe hizo, na akapongeza juhudi za kulinda mfumo huo zilizofanywa na Marais wote wa awamu zilizopita baada ya Waasisi wa Muungano huo kufanya kazi ya kuijenga nchi.

Pia alisema Chama hicho kinakubalika kwa wananchi kutokana kusimamia  misingi ya ukweli na uwazi  unaokubalika Kidemokrasia ndani ya taasisi hiyo unaotokana na utekelezaji wa Ahadi zilizotolewa kwenye kampeni za uchaguzi  Mkuu, zikiwemo utatuzi wa kero za Muungano ambapo hivi sasa kupitia Mwenyekiti wa Kamati ya kushughulikia kero za muungano ambaye ni Makamo wa Rais wa Jamhuri Mh. Samia suluhu Hassan tayari kero 12 kati ya 15 zimetafutiwa ufumbuzi wa kudumu.

Alisema CCM itaendelea kuunga mkono msimamo wa Serikali zote mbili wa kulinda na kutetea Muungano huo kwa  gharama yoyote, ili wananchi waendelee kunufaika na sera na siasa za maendeleo zinazosisitizwa kila mara na viongozi wa chama hicho.

Mwanasiasa huyo na Msomi wa Kada ya Udaktari wa Binadamu, aliahidi kwamba atatumia uwezo aliokuwa nao kwa kushirikiana na viongozi na watendaji wa chama na jumuiya kwa kuisimamia Serikali iendelee kuteleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2015/2020 kwa wananchi waliopo pembe zone hasa Vijijini ili waendelee kupata huduma stahiki.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages