LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 15, 2017

KISWAHILI LUGHA INAYOKUA KWA KASI DUNIANI

Na Genofeva Matemu – WHUSM
Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imeanza kutekeleza malengo iliyojiwekea ya kuifanya Lugha ya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani ili iweze kupata soko na kutumika duniani kote katika kurahisisha mawasiliano ya watumiaji wa lugha hiyo.

Rai hiyo imetolewa na Waziri mwenye dhamana ya Sekta na Utamaduni Mhe. Nape Moses Nnauye alipokua akizungumza na wadau wa Sekta hiyo leo Jijini Dar es Salaam.

“Tumejipanga kuangalia changamoto zinazotokana na Sera na Sheria tulizonazo, changamoto za kirasilimali na mambo ya kiutashi kwani kwa kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo Kiswahili kitaendelea kuwa bidhaa ambayo itavuka mipaka ya nchi na kuitangaza nchi yetu” amesema Mhe. Nnauye.

Akizungumza wakati wa Mkutano huo Katibu Mtendaji Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) Dkt. Selemani Sewangi amewataka waandishi wa vitabu vya Kiswahili kuzingatia weledi wa matumizi fasaha ya lugha ya Kiswahili wakati wa uandishi wa vitabu ili kuweza kuisaidia jamii hasa mashuleni kujua misamiati fasaha ya lugha hiyo.

Kwa upande wake mdau wa Utamaduni nchini Dkt. Musa Hans ameiomba serikali kuhamasisha wageni wote wanaoingia nchini kujifunza lugha ya Kiswahili na kuandaa mwongozo kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu utakaowataka watoto wote wanaoingia sekondari kuwa na kamusi za Kiswahili na kamusi za Kiswahili Kingereza zitakazowasaidia kujua misamihati ya lugha ya Kiswahili.

Naye Mdau wa Utamaduni mama Mipango ameipongeza serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuendelea kutafuta njia mbalimbali za kueneza na kukuza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi.

Katika kuendeleza ukuaji wa Lugha ya Kiswahili Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amekua mstari wa mbele kutumia lugha ya Kiswahili katika shughuli mbalimbali  za kiserikali kama vile Mkutano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Mkutano wa Umoja wa Afrika (AU) ambapo kwa kufanya hivyo lugha hii imeweza kusambaa kwa kasi zaidi. 

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages