LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 23, 2017

SALAM ZA CCM KUTOKA UINGEREZA

CHAGUZI ZA CCM NA MAADUI WAPYA. 
Chama chetu kinakabiliwa na chaguzi mbalimbali za kikatiba mwaka huu 2017.

Yapo mambo mengi yatakachangamana na harakati za chaguzi hizo, lakini kubwa la muhimu ni dhahiri wana CCM wangependa hatimaye ziletwe safu mpya kwenye sura za viongozi wa ngazi zote, yaani kuanzia kwenye Matawi, Wilaya, Mikoa hadi Taifa. 

Na sala hizi (za mabadiliko) za wana CCM zinatokana na aina ya majukumu yaliyopo mbele katika kukabiliana na changamoto mpya zinazopo ndani ya chama na katika nchi yetu sisi kama taasisi ya siasa na pia chama tawala.

 MAJUKUMU:
 CCM lazima ifanye kazi kama taasisi yenye ubora wa hali ya juu  kulingana na mazingira ya sasa. Ubora katika kupanga na kutekeleza (Plan and Deliver) na ili kufanikisha hilo ni lazima chama kiwe makini na wale watakao jitokeza kuwania kujaza nafasi hizo ili kuwabaini kama wanakidhi vigezo vinavyohitajika na kuwa makada wanaoweza kuleta mipango endelevu ya siasa za ccm na hatimaye kusimamia utekelezaji wake pasipo na shaka kwa kutumia raslimali zitakazokuwepo.

Siasa za Tanzania/Africa zinabadilika kwa haraka kutokana na wadau wanaoongezeka (New Generation) ambao mahitaji yao yanabadilika kila wakati na wanatumia nguvu kubwa katika kutaka kuyafikia mahitaji hayo! CCM ni lazima tuwe na safu zinazoweza kumudu kasi hiyo ya mahitaji ya jamii zetu. Lengo kamwe sio kupambana nao bali kutafuta mbinu na nguvu tendaji ya kuweza kutekeleza majukumu ya chama kwa kuzingatia upatikanaji wa matokeo bora.

Matukio kadhaa yaliyojitokeza wakati wa harakati za kumpata mgombea wa uraisi kwa tiketi ya ccm miaka miwili iliyopita yametoa sura halisi kuwa sio wote waliokuwamo kwenye safu mbalimbali za uongozi wa chama chetu walikuwa na vigezo sahihi vya utumishi bora wa chama. 

Wengi wao walijionesha wazi kuwa wapo kwenye nafasi zile kwa bahati mbaya au kwa makusudi ya kujitafutia maslahi binafsi kupitia uongozi wa chama, na pengine walipandikizwa na wapinzani wa ccm ili waweze kuhujumu taratibu za chama!

 Na kasoro za kuwa na viongozi wa namna ile zipo kwenye taratibu za chama chetu hasa katika KUPEMBUA wagombea wa nafasi hizo huko mikoani na hata kwenye jukwaa la taifa. Kamwe ccm isikubali kuendeleza dhana hiyo mbovu katika uchaguzi ujao wa viongozi wa ndani ya chama kwa vyovyote vile. Kama itabainika wagombea waliojitokeza hawana vigezo basi majina yasirudi na uchaguzi uitwe tena au watafutwe wenye sifa hata kama hawakujitokeza kujaza fomu mara ya kwanza.

CHANGAMOTO:
Changamoto tulizonazo kwenye chama ni nyingi kwani sisi ni chama tawala hivyo wajibu wetu ni mpana kuliko wenzetu. Lakini kwanza nianze kwa kubainisha mazingira yanayotuzunguka na hapa nitazungumzia mazingira ya nje ya chama.
Chama kimepata Mwenyekiti mpya (Raisi wetu JPM) hivyo changamoto zimeongezeka kutokana na aina ya utendaji wa kazi wa kiongozi wetu huyo. 

Wapo pia maadui wapya walioongezeka kutokana na sababu hiyo hiyo ya aina ya msukumo (influence) aliyokuja nayo. Zipo pia sababu za kimaumbile ya siasa za nchi yetu na majirani zetu, na hata muungano wetu na mstakabali wake. Kwa leo nitajikita katika dhana mpya ya ujenzi wa uchumi wa VIWANDA, ambayo ndiyo agenda kuu ya Mhesh. Raisi kwa sasa na wapo tunaomuunga mkono na wale wanaopinga kwa sababu zao za kawaida kabisa. 

Kuna wengine wanapinga kwa sababu wamezaliwa nchi ikiwa haina viwanda hivyo wanaona kama ndoto isiyotekelezeka, Lakini tulio watu wazima tunakumbuka viwanda vingi vilivyokuwepo hapo zamani katika nchi yetu hivyo hatuna shaka kuwa inawezekana kabisa kuvijenga upya ikizingatiwa kuwa kuna jukumu pia la sekta binafsi katika azma hiyo ambayo itapunguza nakisi ya utendaji mbaya katika uendeshaji wa viwanda hivyo.

Lakini lengo langu kubwa ni kutoa dokezo ambalo kwangu ni dhahiri ndio nguvu kubwa isiyoonekana katika kuhakikisha kuwa dhana ya viwanda nchini haisongi mbele, Nguvu hiyo haitoki ndani ya nchi pekee bali ipo nje ya mipaka yetu pia. 

Tukumbuke kuwa wakati wa ujamaa adui yetu alikuwa wale viongozi waliokuwa wanajilimbizia mali, sasa kwenye uchumi wa viwanda adui sio huyo tu, bali pia ni yale makampuni makubwa yaliyokuwa yanazalisha bidhaa nje ya nchi/jirani zetu na kuzileta kwetu kama soko. 

Hizo kampuni hazijalala usingizi toka Mhesh. Raisi aweke wazi kuwa nchi yetu sasa inaingia kwenye ushindani wa viwanda. Na makazi zao zinaweza kuwa ni nchi jirani zetu ila watatumia influence mbalimbali za ndani ya nchi ili kuyumbisha lengo hilo(distraction). Watafanya hivyo kwa kupenyeza vijisenti kwa watu wasiotutakia mema na kujenga dhana potofu ikiwemo ya uhaba wa chakula, tetemeko,udikteta n.k 

Kwa hiyo majukumu ya chama kwa sasa ni lazima yaongezeke na kuwa na sura ya uelewa wa kimataifa kwani wabaya wetu hao wataingia hadi kwenye mikoa yetu ambako tunataka kuwekeza viwanda na kwa vile ni dhahiri viongozi wetu wa mikoa wa chama na serikali watahusika kwa namna moja au nyingine katika michakato husika na kama hatutakuwa makini huenda watatumika kuyumbisha dhana hii tukufu ya uchumi wa viwanda. Hivyo kuna kila sababu ya chama kujipanga kiutendaji ili kiweze kuwa mhimili wa mapinduzi haya ya viwanda.

Wanaccm wenzangu mnapoona Raisi anapigwa madongo si kwa sababu ameshindwa kutekeleza kazi zake za uraisi la hasha, bali inawezekana kabisa ni kumyumbisha ili apunguze umakini (focus) kwenye dhana ya viwanda na uchumi mpya visiwezekane chini ya chama cha mapinduzi.

Sisi kwenye matawi ya nje tunafuatilia nyendo hizi kwa karibu sana na hatutakubali upotoshaji unaotumia mitandao ya kijamii.

Kidumu chama cha mapinduzi.

Kangoma H.Kapinga
Mwenyekiti-CCMUK.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages