LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Oct 20, 2016

KAMATI YA BUNGE YAENDELEA KUUJADILI MUSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI

Na Mwandishi Wetu
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imeendelea na kikao cha kujadili Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 kwa kupitia kifungu kwa kifungu kwa ajili ya kuboresha Muswada huo.

Akizungumza leo mjini Dodoma, baada ya kumalizika kwa kikao hicho Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Mhe. Peter Serukamba alisema kuwa baada ya kuwapa wadau muda wa wiki moja kuwasilisha maoni yao juu ya Muswada, wao kama kamati wanaendelea na majukumu yao ya kutunga sheria.

“Sisi kama Kamati tunaendelea na majukumu yetu ya kutunga hii sheria na tumeanza kupitia kifungu kwa kifungu ili kuangali namna bora ya kuuboresha muswaada huu.’’ alisistiza Mhe. Serukamba.

Mhe. Serukamba ameongeza kuwa majadiliano yao sio mwisho wa kutungwa kwa sheria hiyo bali baada ya hapo watakutana na wadau wa habari au kupitia maoni ya watu mbalimbali yaliyowasilishwa kwa njia ya maandishi ili kuiboresha zaidi sheria hii.

Kwa upande wake Mbunge wa Kakonko Mhe. Kasuku Bilago alisema kuwa Muswada huo bado unahitaji kufanyiwa marekebisho na wao kama wajumbe wa Kamati wanaendelea kuupitia Muswaada huo kwa makini kwa kuuchambua kila kipengele na hatimaye kupata Sheria iliyo bora.

“Hatutungi Sheria kwa manufaa ya Serikali sisi wabunge tunatunga Sheria kwa ajili ya wananchi kwahiyo tuzingatie sana maoni ya wadau ili kupata Sheria itakayoleta madadiliko katika Tasnia ya Habari nchini” alisema Mhe. Bilago.

Naye Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Ruvuma Mhe. Sikudhani Chikambo alisema muswada huo ni tofauti na miswada iliyoletwa kipindi cha nyuma kwani umeboreshwa na kwa kiasi kikubwa umezingatia maoni ya wadau wa habari ambao ndio wahusika wakuu wa muswada huu.

“ Muswada huu utawaweka waandishi wa habari katika sehemu nzuri za kujua ukomo wa majukumu yao na kuzingatia weledi na kufuata taratibu na sheria katika kutekeleza majukumu yao alisema,””  alisema Mhe. Sikudhani.

Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii inaendelea na majukumu yake ya kujadili, kuchambua na kuboresha Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 kesho kabla ya hatua nyingine
 Katibu Mkuu Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Prof Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo mbele ya Kamati ya kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii katika kikao cha majadiliano ya Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari leo Oktoba 20,2016 Mjini Dodoma
 Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Anastazia Wambura (kulia) akifuatilia majadiliano kuhusu Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari kati ya Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na Wizara yake leo Oktoba 20,2016 Mjini Dodoma.
 Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Tulia Ackson (kushoto) akifuatilia majadiliano kuhusu Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari kati ya Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na Wizara husika leo Oktoba 20,2016 Mjini Dodoma.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii akifuatilia majadiliano kuhusu Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari kati ya Kamati hiyo na Wizara husika leo Oktoba 20,2016 Mjini Dodoma. Picha zote na Idara ya Habari MAELEZO

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages