LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Sep 30, 2016

GAVANA BENNO NDULU ASEMA KASI YA UKUAJI WA PATO LA TAIFA WAONGEZEKA

GAVANA WA BENKI KUU NDULU
Na Abushehe Nondo na Lilian Lundo, Maelezo.
Kasi ya ukuaji wa pato la Taifa  kwa nusu ya kwanza ya mwaka yaani Januari mpaka Juni 2016 imeongezeka na kufikia asilimia 6.7 ikilinganishwa na asilimia 5.7 kwa nusu ya kwanza ya mwaka  2015.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Benno Ndulu alisema kuwa kwa mujibu wa takwimu kutoka Ofisi  ya Taifa ya Takwimu , hali ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania imeendelea kuwa ya kuridhisha  ambapo katika robo ya pili ya mwaka 2016 ukuaji wa Pato la Taifa unakadiriwa kuongezeka kwa asilimia 7.9 ikilinganishwa  asilimia 5.8 kwa kipindi kama hicho  mwaka 2015.

Ndulu alisema kuwa shughuli za kiuchumi ambazo zimesaidia kukua kwa uchumi katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2016 kuwa ni pamoja naUsafirishaji na uhifadhi wa mizigo asilimia 30.6, uchimbaji wa madini asilimia 20.5, Mawasiliano na Habari asilimia 12.6 na Sekta ya fedha na Bima asilimia 12.5.

Alisema ukuaji wa sekta ya uchukuzi na ujifadhi wa mizigo umetokana na kuongezeka kwa usafirishaji wa abiria kwa njia ya biashara na gesi asili ambao umekua kwa zaidi ya nusu ukilinganisha na robo ya pili ya mwaka 2015 kwa asilimia 9.4.

Akizungumzia hali ya ukuaji wa uchumi kwa nusu ya mwaka 2016 Ndulu alisema kuwa katika nusu ya kwanza ya  Januari hadi Juni mwaka 2016 kasi ya ukuaji wa pato la Taifa umeendelea kukua kwa kasi kutokana na baadhi ya sekta kuonekana kukua zaidi ikiwemo Uchukuzi na Uhifadhi wa Mizigo asilimia 17.4

Sekta nyingine ambayo imekua kwa kasi kwa kipindi hicho ni pamoja na sekta ya Uchimbaji wa Madini na Gesi asilimia 13.7, Mawasiliano asilimia 13.0 na sekta ya fedha na Bima asilimia 13.0.

Akifafanua michango ya shughuli mbalimbali zilizochangia ukuaji wa  kiuchumi  katika nusu ya kwanza ya Mwaka huo alizitaja kuwa ni pamoja na Uchukuzi na Uhifadhi  Mizigo asilimia 16.0, Ujenzi asilimia 10.7, na Sekta ya Kilimo ambayo inaonekana kukua kwa asilimia 10.3 katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016.

Aidha alisema kuwa kwa kuangalia hali ya ukuaji wa pato la Taifa kwa nusu ya kwanza ya mwaka pamoja na viashiria mbalimbali vya uchumi ni mategemeo yao kwamba pato la Taifa kukua kwa asilimia 7.2 kwa mwaka 2016 litafikiwa. 

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages