LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Apr 16, 2016

JULIUS MTATIRO, HUJAELEWA MAANA YA KUFUFUA VIWANDA


 
Na Ally S. Hapi

Kwanza naomba nitofautiane sana na mwanachuo mwenzangu (University mate) na Waziri Mkuu wangu wa zamani DARUSO Mlimani bwana Julius Mtatiro kuwa nimesikitishwa sana na makala yake kuhusu viwanda.  Hasa pale alipoonesha kwa bahati mbaya au makusudi uelewa finyu juu ya jambo hili la kufufua viwanda nchini.
Napenda kumkumbusha historia Mtatiro kuwa mfumo wetu wa Uchumi kabla ya kuja kwa sera ya ubinafsishaji ulikua mfumo hodhi wa uchumi (Ujamaa), ambapo serikali ndiyo ilimiliki na kuendesha njia zote kuu za uzalishaji mali vikiwemo mabenki na viwanda. Serikali katika mfumo ule wa uchumi  (Ujamaa) ilikua inamiliki viwanda kama Caltex, Sunguratex, Mwatex na vingine vingi Na ilikua ikifanya biashara.

Baada ya kuja kwa mfumo mpya wa uchumi (Uchumi wa soko) hasa baada ya masharti ya benki ya dunia kupitia Structural Adjustment Programmes (SAPs), miaka ya mwishoni mwa 1980 na hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990 nchi yetu na nyingine zilizokua zinafuata mfumo kama wetu wa uchumi zilipaswa kujiondoa katika serikali kumiliki njia kuu za uzalishaji mali na kufanya biashara na hivyo kuruhusu sekta binafsi kufanya kazi hiyo. Serikali zikapaswa kubaki na eneo la huduma tu (service). Hapa ndipo ulipokuja "Ubinafsishaji". Mashirika kama NBC, viwanda na mahoteli vilibinafsishwa wakati huu.

Wakati wa Ubinafsishaji miaka ya 1990, viwanda vyote vilivyokua vya serikali pamoja na mabenki vikapewa kwa wawekezaji binafsi ili waviendeshe. Hivyo huu ndio ukawa mwisho wa serikali kuanzisha na kuendesha viwanda. Viwanda vyote vipya vilianzishwa na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Hivyo basi, kwa mantiki hiyo na historia hiyo, agenda ya kufufua viwanda haina maana ya serikali kujenga na kuendesha viwanda. La hasha. Wala haina maana ya serikali kutenga bajeti ya kujenga viwanda, la hasha.

NINI MAANA YA AGENDA YA  KUFUFUA VIWANDA?

Napenda kuendelea kumuelimisha bwana Mtatiro kuwa, bajeti ya shilingi Bilioni 95 ya Wizara ya Viwanda na biashara hailengi kutumika kujenga viwanda, maana hilo si jukumu la serikali katika uchumi wa soko.
Maana ya agenda ya kufufua viwanda ni hii ifuatayo:-

1. Kurejesha serikalini na kuwapa wawekezaji wengine viwanda vyote ambavyo wale waliobonsfsishiwa walishindwa kuviendesha kwa mujibu wa masharti waliyopewa. Wengine wanavitumia kufuga mbuzi na wengine wamevifunga kabisa. Ikumbukwe kuwa watu waliobinafsishiwa walipewa masharti maalum.

2. Kuhkikisha serikali inaboresha mazingira mazuri kwa ajili ya wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili wavutike kuja kuwekeza katika nchi yetu. Hili linaweza kufanywa kwa njia zifuatazo:

a. Kuondoa urasimu katika mfumo wetu wa serikali hasa kwenye uanzishwaji wa viwanda, upataji wa leseni n.k.

b. Kuboresha miundombinu muhimu ya barabara na reli ili kurahisisha usafirishaji bidhaa na malighafi kutoka na kwenda viwandani

c. Kuhakikisha nchi inakua na umeme wa kutosha na wa uhakika. Viwanda vinahitaji umeme mwingi sana.

d. Kuweka masharti nafuu kwa waanzishaji wa viwanda vipya ili kuwahamasisha watu kuwekeza.

e. Kuimarisha sekta ya Kilimo cha kisasa na ufugaji wa kisasa ili kuhakikisha upatikanaji wa malighafi ya kulisha viwanda kutoka ndani ya nchi. Viwanda muhimu na vya mwanzo katika mapinduzi ya viwanda ni vile vya mazao ya Kilimo (Agriculture Support Industries) kama vile viwanda vya nguo, nyama, mbolea, sementi, maziwa, mafuta ya kula, nta, ngozi, vifungo n.k.
Hivi ndivyo viwanda vya mwanzo ambavyo vina umuhimu mkubwa katika kufufua uchumi wa nchi kwakua vinaajiri watu wengi na vinafufua na kukuza Kilimo na Ufugaji.

f. Kuzitangaza fursa za viwanda zilizopo nchini kupitia njia za mawasiliano za kisasa, Kituo cha Uwekezaji Tanzania  (Tanzania Investment Centre )na kupitia balozi zetu.

g. Kutenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda katika mikoa yetu na kuyaweka katika kitabu maalum ili iwe rahisi kwa wawekezaji wa ndani na nje kujua wapi pana fursa gani ya kuanzisha viwanda. Maeneo haya yaunganishwe na miundombinu muhimu kama umeme, maji na barabara.

h. Kuweka sera, sheria na mikakati kabambe kwa ajili ya utekelezaji wa hayo.

UFUFIAJI VIWANDA NI SUALA MTAMBUKA

Kwa maelezo hayo hapo juu ni dhahiri kuwa suala au agenda ya kufufua viwanda sio agenda ya Wizara ya Viwanda na biashara pekee. Ni suala la wizara nyingi kufanya kazi pamoja na kwa mafungamano (interconnectedly).
Ni suala la wizara ya nishati, kilimo, viwanda, fedha, mambo ya nje n.k.

Pili, ni dhahiri kuwa hesabu za bwana Mtatiro za (bilioni 100 × miala 5 = bilioni 500)katika kufufua viwanda ni hesabu potofu za mtu ambaye hana uelewa wa kutosha wa masuala ya viwanda na uchumi. Hivyo namshauri rafiki yangu huyu aendelee kufanya utafiti zaidi ili siku nyingine aandike mambo ambayo ana uelewa nayo.

USHAURI KWA WIZARA

Tatu, niwaombe na kuwashauri watu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, hasa waziri Mwijage na Katibu Mkuu wake, mbali na kuja na bajeti ya wizara ya mwaka 2016/2017, hawana budi kuja na Kijitabu Cha Mkakati wa Kufufua Viwanda nchini  (MKAKUVI) ambacho kitaeleza kwa kina ni kwa vipi na kwa namna gani Serikali inakwenda kufufua viwanda nchini. Aidha mkakati huo uainishe fursa zote za viwanda zilizopo nchini na namna serikali ilivyojipanga katika kuzitangaza fursa hizo kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi. Hii ni katika kutekeleza dira iliyotangazwa na Mh. Rais ya kujenga taifa la viwanda.

Ally. S Hapi

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages