LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 19, 2015

HOJA MTAMBUKA: LOWASSA ANAPOFUATA NYAYO ZA MYAHUDI WA KWANZA KUSWALISHA WAISLAM

NA BASHIR NKOROMO
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete baada tu ya kuingia ukumbini kwenye kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) Juni 11, 2015, katika Jengo la White House, mjini Dodoma, alitamka "Haijapata kutokea".

Tangu siku hiyo, Watanzania wamekuwa wakipigwa na butwaa na hakika waacheni wapigwe na butwaa, waacheni wajae kwenye mikutano yake wakimshangaa kwani haijapata kutokea katika historia ya Tanzania na Afrika.

Kama inavyofahamika tangu enzi na enzi, ni vigumu sana kwa Myahudi kuswalisha katika msikiti wa Waislam, kama ilivyokuwa kwa Kiongozi wa chama cha CUF kuisimamia Ilani ya Uchaguzi ya TLP, lakini wapo wayahudi kadhaa wamewahi kufanya hivyo.

Kwa kawaida watu hununua wanasiasa, wakawatumia kwa maslahi yao, kuwasemea ajenda zao, na sina uhakika kama kuna anayebisha kuwa hakuna wanasiasa waliowahi kununuliwa hapa Tanzania, hasa ikizingatiwa kwamba kununuliwa kwenyewe kuna namna nyingi ambazo sidhani kama inafaa kuzitaja hapa kwa sababu zote zinajulikana.

Lakini katika historia ya Tanzania na Afrika ni mwanasiasa mmoja pekee, ndiye ameonyesha kuweka historia ya kununua Chama cha Siasa kizima kizima, na hakuishia hapo akanunua pia Muungano wa vyama vya siasa ili asimame kama mgombea, na amefanikiwa, haijapata kutokea.

Historia hii ya kipekee ilitanguliwa na mtu mmoja tu, anaitwa Giovanni Leone, ambaye alikuwa Kiongozi wa Chama cha Wakristo cha Italy ( DEMOCRAZIA CRISTIANA au CHRISTIAN DEMOCRACY) ambaye hakuwahi kuwa mkristo, lakini akaweka historia ya kuwa kiongozi wa Wakristo ambaye hakuwa Mkristo.

Giovanni Leone aliingia madarakani kama Waziri Mkuu, mnamo Juni 21, mwaka 1963 na kujiuzulu miezi sita baadae, yaani Desemba 4, mwaka huo huo wa 1963 kwa kashfa ya Ufisadi.

Mwaka 1968, aliingia tena madarakani baada ya kununua Muungano wa vyama vya upinzani Italy, ulioitwa THE PENTAPARTITO ambao uliundwa na vyama vitano ambavyo ni PSI, PSDI, PRI, PLI na DC.

Hata hivyo, kama ambavyo waswahili husema, kwamba maji hata yachemke hipi hayasahau baridi au jasiri haachi asili, Bwana Leone alidumu madarakani kwa miezi sita tena kwa maana kuanzia Juni hadi Desemba 22,1968, Bunge lilipomuondoa kutokana na matumizi mabaya ya nafasi yake kama Waziri Mkuu wa Italy.

Licha ya kuvunja rekodi Giovanni Leone ameacha fundisho duniani, kwamba mtu hata ajaribu vipi kuwa jasiri akaweka historia ya kufanya yasiyowezekana katika masuala ya uongozi, hatima yake huwa hafiki mbali.

Mwanachama wa juzi juzi tu wa Chadema ambaye ndiye pia mgombea Urais kwa tiketi ya chama hicho, 'kilichoviweka kwapani' pia vyama vya CUF, NCCR Mageuzi na NLD, Waziri Mkuu aliyejizuru kwa kasha ya Richmond, Edward Lowassa ni kama ameamua kufuata nyazo za Giovanni Leone, kitabia na mwenendo wake kisiasa.

Ni wazi ukiutazama mtiririko wa kitabia na kisiasa hadi alikofikia sasa, itakuwa vigumu kwa Lowassa kufuata misingi asiyoijua ya Chadema na UKAWA, na pia itakuwa vigumu kutekeleza ILANI asiyoijua wala kushiriki kuiandaa na itakuwa vigumu kwake kuamini katika UKAWA au CHADEMA kwani kwake Chama hicho ni kama Baba wa kufikia.

Ni kwa sababu hizo, ndiyo Watanzania wengi wanaendelea kumshangaa Lowassa kwa sababu HAIJAPATA KUTOKEA kada kindaki ndaki wa CCM kuwa JEMEDARI wa wapinzani!

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages