LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Mar 17, 2015

WANAUME NA WAVULANA WADAU MUHIMU KUFIKIA USAWA WA KIJINSIA

Na Mwandishi Maalum, New York
Mkutano  wa 59 wa Kamisheni  kuhusu  Hadhi ya Wanawake ( CSW) umeingia wiki  ya pili  ambapo wajumbe  wameendelea kujadiliana na kubadilishana   uzoefu kuhusu mada mbalimbali zinazohusu hadhi ya  mwanamke na mtoto wa kike.

Jana Jumatatu  miongoni mwa majadiliano  ambayo yamevutia  wajumbe wengi  yalihusu wajibu wa wanaume na wavulana katika kufikia usawa wa kijinsia.

Katika majadiliano hayo ilielezwa kwamba ili kufikia usawa wa kijinsia,  basi  hapana  budi kuhakikisha kwamba wanaume na wanavulana wanashirikishwa  kikamilifu katika safari hiyo.

Imeelezwa  katika majadilianao hayo kuwa Ushiriki wa wanaume na wavulana  kutaongeza kasi ya kufikiwa kwa usawa wa kijinsia, na kwamba  jukumu hilo haliwezi likawa la wanawake  peke yao.

 Baadhi ya nchi zilichangia  uzoefu wao wa namna gani  zinatekeleza  dhana hiyo ya kuhakikisha kwamba wanaume na  wavulana  wanatimiza wajibu wao kwa   kuhakikisha kwamba  jamii  yote inakuwa na uelewa na ushiriki sawa katika  kufikia lengo la kuwa na usawa wa  jinsia.

Pamoja na   majadiliano kuhusu mada hiyo, wajumbe wanaoshiriki mkutano huu  pia wameendelea na  majadiliano ya mada  nyingine nyingi zilizokuwa zinafanyika katika kumbi mbalimbali za mikutano hapa Umoja wa Mataifa.

Baadhi ya  mada hizo ni ile iliyohusu : kubadlisha kanuni za jamii,  ili kufikia usawa wa kijinsia, matarajio  na fursa.

Ajenda kuu ya  Mkutano  wa 59 wa Kamisheni kuhusu  hadhi ya wanawake,  unaohudhuriwa na  wajumbe   kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa,  Taasisi za UM na  wawakilishi kutoka Asasi Zisizo za Kiserikali, ni Azimio la  Beijing na  Jukwaa la utekelezaji,  miaka 20 baada ya kufanyika mkutano wa  nne wa kihistoria wa wanawake, mkutano uliofanyika mwaka 1995 Beijing, China.

Kupia Ajenda hiyo  ya   Beijing+20) wajumbe wanajadili  changamoto za utekelezaji wake na mafanikio katika   usawa wa kijinsia na uwezeshaji  wa wanawake.

Wajumbe pia wanajadili matokeo ya kikao maalum cha 23 cha Baraza Kuu  la Umoja wa Mataifa, tathmini  ya miaka mitano baada ya kupitishwa kwa jukwa la utekelezaji, tathmini iliyoainisha hatua Zaidi na mipango  inayotakiwa kutekelezwa  ili kufika  lengo la usawa wa kijinsia na uwezeshaji.

Vile vile mkutano huu  unajadili fursa kwaajili ya kufikia usawa wa kijinsia  na uwezeshaji  kupitia ajenda mpya za maendeleo baada ya 2015.
 Wajumbe wakifuatilia majadiliano kuhusu uwezeshaji wa wanawake, ambazo wazungumzaji wakuu  walikuwa ni Balozi Tuvako Manongi,  Waziri K. Kellie kutoka Canada  na Waziri Asa Regner kutoka Sweden katika mchango wake, Balozi Manongi alisema mifuko ya uwezeshaji ambayo imeanzishwa nchini Tanzania ni  moja ya  mafanikio ambayo  imeweza kuwakwamua wanawake kuondokana na  umaskini.   Baadhi ya mifuko hiyo ni  Mfuko wa  Maendeleo  ya Wanawake kwa Tanzania Bara na  Mfuko wa  Maendeleo  ya wanawake  wajasiriamali Tanzania Visiwani.pia alielezea miradi mbalimbali ya uwezeshaji wa wanawake ambayo  inafadhiliwa na wadau wa maendeleo kama vile Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji ya Umoja wa  Mataifa ( UNCDF) unaofadhili  mradi wa kuzalisha umeme  huko  Mkoani Iringa. Majadiliano hayo yaliandaliwa kwa ubia wa UN- Women,  UNCFD na  UNDP
 Mawaziri Mhe. Zainabu Omar Mohammed, kutoka Serikali ya Mapunduzi Zanzibar na  Mhe Sophia Simba kutoka Serikali ya Muungano wakiwa na mwenyeji wao  Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa Balozi Tuvako Manongi.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages