LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jul 21, 2014

NAPE: WANAOTAKA URAIS 2015 RUKSA KUTANGAZA NIA, KUPIGA KAMPENI KOSA LA 'JINAI'

NA BASHIR NKOROMO
CCM imeweka wazi kwamba kwa mujibu wa taratibu zake, wanaotaka urais kupitia chama hicho wako huru kutangaza nia, na kusisitiza kwamba ugomvi wake mkubwa ni kwa wanaofanya kampeni kabla ya wakati.

Imesisitiza kwamba, kitawachulia hatua stahiki kwa mujibu wa katiba na taratibu za chama, bila kuwaonea huruma wala aibu, kutokana na namna yoyote ikiwemo uwezo wa fedha, nafasi zao za uongozi au umaarufu walionao wale wote watakaobainika kutangaza nia na kisha wakafanya kampeni kabla ya muda rasmi, kwa namna yoyote kutaka kuwania kuteuliwa na CCM kuwania Urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani.

Hayo yamesemwa na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, wakati akizungumza katika kipindi cha 'Baragumu' kwenye Kituo cha Televisheni cha Chanel ten, leo Julai 21, 2014, kilichokuwa na mada 'Urais na Makundi ndani ya Chama'.

"kwanza kabisa Chama chetu kina wanachama wengi, tena wenye sifa za uongozi katika nafasi mbalimbali, katika wingi huu wa wanachama kutakuwa na watu wengi wenye uwezo wanaotaka urais na nafasi nyinge za uongozi,  kwa maana hiyo kelele za kutaka zitakuwa nyingi kwa maana na ushindani na ndiyo maana wenzetu huvizia wawili watatu wanaokosa na kuwafanya wagombea wao", alisema Nape.

Nape alisema, wingi na ubora huu wa wanachama kuwa na sifa za kuwania uongozi ikiwemo urais, bado haiwezi kuwa sababu ya kuacha kila mmoja kutafuta nafasi kwa kupitia utaratibu anaotaka yeye, kila anayedhani kuwa anafaa kuongoza kupitia CCM, lazima kuhakikisha anazingatia kanuni za uongozi na maadili na kanuni za uchaguzi ndani ya CCM.

Alisema kwa mujibu wa kanuni ya Uchaguzi za CCM mwanachama anaruhusiwa kutangaza nia, lakini ni marufuku kuita watu na kuwashawishi kwa maneno, fedha au takrima vyote vikiwa na sura ya kampeni.

Nape alisema, lengo la kanuni hizo za chama ni kuzuia makundi ya mapema ambayo husababisha mtafaruku na mgawanyiko mkubwa ndani ya Chama jambo ambalo alisema, chama kinalikemea kwa lengo la kulinda imani na nguvu ya chama.

Alisema, baadhi ya waliotangaza nia ya kuwania Urais na kupewa onyo kali kwa kipindi cha miezi sita, baada ya kubainika kufanya kampeni kwa namna moja au nyingine,wasipojirekebisha, kwa mujibu wa kanuni wataongezewa adhabu ya karipio kali adhabu ambayo ni ya miezi 18, ambapo utekelezwaji wake utamfanya mhusika kukosa sifa ya kuwania uongozi wa ngazi yoyote kupitia Chama.

Nape alitoa mwito kwa wanaotaka kuwania uongozi hasa urais kwa tiketi ya CCM, kujitahidi kuzingatia kanuni na taratibu zilizopo, ili wasije wakapoteza sifa ya kuwania nafasi wanazotaka.

"Tena, mimi nawaambia hawa, waache kujaribu kujenga makundi kabla ya wakati kwa sababu hata wao hawatanufaika, maana hata wakija wakapata kuteuliwa huku CCM ikiwa vipande vipande hawatapata wanachotaka", alionya Nape.

Akizungumzia sifa za kuwania Urais, Nape alisema, zinazozingatiwa na chama ni zile zilizopo hata kwa mujibu wa Katiba ya nchi, na siyo vigezo vingine kama baadhi wanavyojaribu kutaka kubebwa kupitia ukanda, jinsia, hali au umri.

CCM NI MZAZI HALALI WA MUUNGANO, NI KAZI YA MIKONO YAKE, LAZIMA IUPIGANIE USIFE
Akizungumzia vuguvugu la kutafuta katiba mpya, Nape alisema mchakato wa kaptiba mpya hauzuii maisha kuendelea na ndiyo sababu shughuli nyingine zinaendelea.

Alisema, licha ya shughuli nyingine kuendelea, suala hilo la Katiba mpya CCM imelipa umuhimu wa kutosha kuhakikisha ushiriki wake kama chama utatoa katiba yenye manufaa kwa Watanzania wote.

Nape alisema, madai ya wapinzani kwamba Bunge la Katiba halijadili rasimu ya wananchi ni kivuli cha ajenda yao binafsi lakini ukwli ni kwamba kinachojadiliwa ni rasmu halali ambayo iliwasilishwa na tume ya Katiba.

"Hawa jamaa wanapodai kuwa kinachojadiliwa siyo rasimu ya Katiba, sasa kinachojadiliwa ni nini?, mbona wabunge wameshajadili sura ya kwanza na ya sita ya rasimu hiyo, sasa hawa wanataka kutuambia kwamba mabilioni ya fedha yanayotumika ni ya nini na kwa faida gani", Nape alisema na kuhoji.

Nape alipuuza pia wapinzania wanasema Bunge la Katiba halina mamlaka huku wakijua kwamba kanuni zinazolipa mamlaka bunge hilo, zimetungwa humo humo kwenye bunge la Katiba na wapinzani wenyewe akiwemo Mbunge wa Chadema, Tundulisu Lisuusa.

Kuhusu muundo wa muungano katika mchakato huo wa Katiba, Nape alisema, kinachopiganiwa ni maslahi ya wanasiasa kutaka nafasi za uongozi, lakini ndiyo sababu wapinzania wanafikia zaidi muundo wa serikali tatu ambao kwa vyovyote utaua Muungano.

Nape alisema, baada ya kuona CCM ni wamoja sana kwenye suala la maslahi ya kulinda iliouchojenga kwa miaka 50, wapinzania wameanzisha kikundi walichokiita Umoja wa Katiba ya wananchi- Ukawa,a mabcho alisema, ni 'kijikundi' kidogo tu japo kina kilele sana, kwa kudhani wataweza kupata njia ya mkato.

"Muungano japokuwa ni wa Watanzania wote ni kazi halali ya miko  CCM, yeyote anayeleta chochote kinachotaka kuua muungano huu tutashughulika naye kwa hoja na nvugu zetu zote", alisema Nape.

Akizungumzia hoja ya Rais Jakaya Kikwete kutoa maoni yake kwamba serikali tatu ndiyo mfumo utakaouweka salama muungano, Nape alisema, Rais alitoa hilo kama mlezi wa nchi lakini wabunge wa bunge la Katiba hawakuzuiliwa kujadili kwa kina rasim kadri watakavyoona inafaa kwa faida ya taifa la Tanzania.

"Mimi nampongeza Rais Kikwete, kwa sababu kama kiongozi mkuu wa nchi ni kama baba ndani ya nyumba, ilimpasa kutoa angalizo lake lakini pia akatoa uhuru kwa wabunge kuamua watakavyoona inafaa, kufuata ushauri wake au kuuacha", alisema Nape.

Alimsifu Rais Kikwete kuwa ni kiongozi muungwana sana, akisema, kwamba, angekuwa Rais dikteta angeweza kuielekeza Tume ya Katiba chini ya jaji na Waziri Mkuu mstaafu Joseph Warioba, kufuata maelekezo yake kwa kuondoa kwanza asiyo yataka kabla ya rasimu kupekwa kwenye Bunge la Katiba.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages